Saturday, April 21, 2012

NIFANYE NINI ILI KUSHINDA TAMAA ZA MWILI?



NIFANYE NINI ILI KUSHINDA TAMAA ZA MWILI?

Na: Patrick Sanga
Septemba mwaka huu, Mwanafunzi mmoja wa shule ya Sekondari alinitembelea nyumbani kwangu hapa Dodoma. Alipofika nilimkaribisha ndani nikajua amekuja kunisalimia tu. Baada ya muda akaniambia kaka Sanga nina swali nahitaji msaada wako sana. Tukatoka nje mahala penye utulivu ndipo akaniambia tamaa za mwili kwa maana ya uasherati/zinaaa zinanitesa nifanye nini ili kushinda? Jambo hili linanitesa kiasi kwamba nahisi kama vile sijaokoka kutokana na vita niliyonayo katika fahamu zangu na mwilini mwangu?
Kwa kuwa vijana wengi wamekuwa wakiuliza swali hili kwa namna tofauti tofauti na kwa njia mbalimbali, nimeona ni vema nikaliweka somo hili kwenye ‘blog’ hii  kwa kuwa tunao vijana wengi ambao changamoto hii inawakabili pia. Naam yafuatayao ni mambo ya msingi kuzingatia ili kijana aweze kuwa na ushindi dhidi ya tamaa za  mwili (dhambi) nk.
  • Kwa kutii na kulifuata neno la Mungu
Biblia katika Zaburi 119:9 inasema ‘Jinsi gani kijana aisafishe njia yake? Kwa kutii, akilifuata neno lako’. Ukisoma Mstari huu katika tafsiri ya Biblia ya Kiingereza ya GNB unasema How can young people keep their lives pure? By obeying your commands’. Mtazamo wa tafsiri hii ya kiingerza ni kujaribu kutafuta ufumbuzi wa namna ambayo vijana wanaweza kuishi maisha ya utakatifu na yenye ushuhuda. Inawezekana mwandishi huyu wa Zaburi aliona namna vijana wanavyohangaika katika eneo hili, ndipo ikabidi amuulize Mungu, ni jinsi gani kijana aisafishe njia/au anaweza kusihi maisha ya utakatifu? Kipengele cha pili kinatupa jibu la swali la kwanza kwamba ni kwa kutii, akilifuata neno lako.
Naam hii ina maana ni lazima kwanza kijana achukua hatue  ya kuliweka neno la Mungu moyoni mwake kwa wingi, maana hawezi kutii neno ambalo halimo ndani yake au hajalisoma na kulitafakari. Zaburi 119:11 inasema ‘Moyoni mwangu nimeleiweka neno lako, Nisije nikakutenda dhambi’. Maana yake ni kwamba, kama kijana atajijengea tabia ya kuhakikisha analiweka neno la Bwana moyoni mwake kwa kulitafakari kila siku, kwa vyovyote vile lazima atakuwa na ushindi dhidi ya tamaa za mwili na kazi zote za Shetani. Naam usiishie tu kuliweka moyoni mwako bali fuatilia sauti ya neno uliloliweka ndani yako, ukaiitii.
  • Kuacha michezo ya mapenzi na kuwa makini na nini unatazama/unasikia.
Michezo ya mapenzi (foreplay) ni maalumu kwa ajili ya wanandoa. Kwa bahati mbaya vijana wetu nao sasa wamekuwa wakifanya mambo haya ambayo kimsingi si yao. Michezo ya mapenzi ni sehemu ya vitendo vyvyote ambavyo hupelekea ashiki ya kufanya tendo la ndoa hii ni pamoja na kushikana shikana/kugusana maeneo mbalimbali ya mwili na pia kunyonyana ndimi.
Zaidi Katika dunia ya sasa Shetani ametumia teknolojia iliyopo kuteka fikra za vijana wengi. Vijana wengi kupitia simu, computer, video nk wanaangalia picha chafu za ngono na kusoma jumbe za aina hiyo kitu ambacho kinaharibu fahamu zao bila wao kujua. Na kwa kufanya hivyo wanakuwa wanayachochea mapenzi na kuamsha tamaa zao za mwili. Naam mambo haya ni hatari tena kinyume na mapenzi ya Mungu. Na kwa bahati mbaya vijana wetu tena waliokoka baadhi yao bado wamefungwa katika kufanya mambo haya.
Katika kile kitabu cha Wimbo Ulio Bora 2:7 Biblia inasema ‘Nawasihi, enyi binti za Yerusalemu, Kwa paa na kwa ayala wa porini, Msiyachochee mapenzi, wala kuyaamsha, Hata yatakapoona vema yenyewe’. Kulingana na mstari huu tunajua kwamba, kumbe mapenzi yanaweza kuchochewa na kuamshwa, naam na hili ni jambo hatari sana kama litafanywa na wahusika ambao si wanandoa kwa maana ya (foreplay) hata kama wana kiroho cha iana gani.
Jambo la msingi kuepuka hapa ni kuwa kwenye mazingira ambayo yanaweza yakawashawishi kufanya mambo haya. Vijana ambao si wanandoa kutembeleana mahali wanaposihi kwa maana ya eneo ambalo wako pekee yao, au kwenda guest na  maeneo yote ya namna hii eti kwa lengo la kupanga mipango yenu. Fahamu kwamba kitendo cha vijana wawili ambao si wanandoa kukaa katika mazingira ya aina hii ni kumpa Iblisi nafasi ya kuwamaliza, naam kijana uwe makini usifanye ujinga huu, Shetani asije akakumaliza.
  • Kuenenda kwa Roho.
Mtume Paulo alikutana na kesi ya aina hii kwa wandugu wa kanisa la Galatia. Moja ya ufumbuzi juu ya suala hili aliwataka waenende kwa Roho ili wasisitimize kamwe taamaa za mwili. Wagalatia 5:16 ‘Basi nasema, Enendeni kwa Roho, wala hamtazitimiza kamwe tamaa za mwili’. Kuenenda kwa Roho ndio kukoje? Ni kuishi/kuenenda kwa kufuata utaratibu/uongozi wa Roho Mtakatifu maishani mwako (Zaburi 32:8). Jambo la msingi ni kuwa mtiifu kwa Roho Mtakatifu, naam atakusaidia kushinda dhambi kama alivyomsaidia Bwana Yesu alipokuwa hapa duniani.
  • Kujitenga na marafiki/makundi mabaya
Zaburi 1;1 inasema ‘Heri mtu yule asiyekwenda katika shauri la wasio haki; Wala hakusiamama katika njia ya wakosaji; Wala hakuketi barazani pa wenye mizaha’. Jiulize muda wako mwingi unautumia kwa kufanya nini? Na kama ni marafiki ni marafiki wa aina gani?  Siku zote wale unaokuwa nao karibu wanachangia sana kujenga (kushape) mfumo wa maisha yako. Biblia katika 1 Wakorinto 15:33 inatuambia ‘Msindanganyike; Mazungumzo mabaya huharibu tabia njema’. Naam kama utakuwa na marafiki wabaya basi tegemea na mazungumzo yao yatakuwa mabaya na hivyo tegemea na wewe kuwa na tabia mbaya. Jambo la msingi ni kujitenga nao usiende katika shauri lao, wala njia yao na pia kuketi katika baraza yao.
Mtume Paulo akizungumza na kijana wake Paulo alimwambia hivi ‘Mtu awaye yote asiudharau ujana wako, bali uwe kielelezo kwao waaminio, katika usemi na mwenendo, na katika upendo na imani na usafi’ 1 Timotheo 4:12. Wazo ninalotaka ulipate hapa ni kwamba kama Paulo angejua kwamba vijana hawawezi kuishi maisha ya utakatifu na yenye ushuhuda katika dunia hii, asingemwambia Timotheo afanye haya. Basi kwa kuwa alijua inawezekana, ndiyo maana Roho Mtakatifu alimwongoza kuandika haya ili kumwagiza Timotheo na sisi vijana wa leo katika jambo hili. Naam uwe kielelezo katika shule, chuo, kanisa, kazini nk ili Mungu aone sababu ya kuendelea kukutumia kwa utukufu wake.
Neema ya Mungu iwe nanyi

JIANDAE KUZIKABILI CHANGAMOTO NA KUZITUMIA FURSA ZINAZOKUJA



JIANDAE KUZIKABILI CHANGAMOTO NA KUZITUMIA FURSA ZINAZOKUJA.

 Na: Sanga P.S.
Jiandae kwa sababu mbele yako kuna changamoto zinakuja. Nyingine zimeruhusiwa na Mungu, au wewe mwenyewe kwa kumpa Ibilisi nafasi (Waefeso 4:27). Na bila maandalizi changamoto hizi zinaweza zikaharibu mahusiano yako na Mungu na kupelekea makusudi ya Mungu kupitia wewe kutofanikiwa.
Zaidi nataka ujiandae kwa sababu zipo fursa ambazo Mungu anazileta ili kukufanikisha. Lakini pia zipo fursa ambazo Shetani anazileta na usipokuwa makini nazo zitakuvuruga na kuharibu mahusiano yako na Mungu. Lengo la huu ujumbe ni kukuandaa na kukufunza ujue namna ya kujiandaa kuzitumia fursa ili kukabilana na changamoto mbalimbali zinazokuja.
 Changamoto ni nini?– ni mazingira kinzani, ya upinzani kwenye kila nyanja yanayokuja katika maisha yako. Kwa jina jingine ni matatizo. It is a situation that demands innovativeness, a situation/a trial available to test an organizational/personal capacity/ability.
Kwa hiyo haya ni mazingira/matatizo/vikwazo vinavyojitokeza ili kupima uwezo wa mtu au taasisi/kampuni. Lengo la changamoto ni kukusaidia  uwe mbinifu, mvumbuzi. Changamoto haziwezi kukwepeka kwenye maisha, kwa sababu zimeruhusiwa na Mungu mwenyewe na ndio sehemu ya maisha, soma Mithali 16:4 Ayubu 1:11 Waamuzi 3:1-6   Kumbukumbu 8:1-3
 Fursa–ni nafasi, mlango, uwezo, uwezekano, tukio, muda unaojitokeza/uliopo ili kukuvusha kwenye changamoto inayokukabili.
Fanya maandalizi kwa sababu mbele yako kuna fursa zinakuja ambazo hautakiwi kuzikosa hata moja. Fursa zinakuja ili zikusaidie kukabilana na changamoto ulizonazo. “A big/better opportunity favors the prepared mind”. Hii ina maana fursa inapojitokeza inakuja kuwa jibu la changamoto unayoipitia au itakayokuja kwa hiyo ni vema ukaitumia hiyo fursa vizuri.
Changamoto na fursa ni sehemu ya maisha ya mwanadamu kutoka kwa Mungu. Si watu wengi wanaojua kuzitumia vizuri fursa ambazo Mungu amezileta kwenye maisha yao. Ngoja nikueleze siri hii, kila mwaka una changamoto na fursa zake. Sasa unatakiwa kujiandaa ili kukabiliana na changamoto na kwa kuzitumia fursa  husika.
Mifano ya watu walioshindwa kuzitumia vizuri fursa zao. Soma habari hii katika Luka 19: 41-44. Ukisoma hii habari utaoona jinsi Yesu alivyoulilia mji wa Yerusalemu kwa kushindwa kuzitumia fursa ambazo alizitengeneza kwao lakini wao wakashindwa kuzitumia.
Kosa la Jerusalem ni kutokujua muda wa kujiriwa kwake.. “All this will happen to you because u did not know the time of your salvation”. Kumbuka tulikotoka muda ni fursa Kumbe kuna magumu, mabaya, matatizo yanatupata kwa sababu tu hatujajua namna ya kuzitumia fursa zilizopo mbele yetu.
Hebu tujifunze kutoka kwa nabii Haggai 1:3-11. Soma pia habari hii vizuri. Kosa la watu wa kkipindi cha nabii Hagai ni kusema huu si muda wa kujenga nyumba ya Bwana bali za kwetu. Kwa kuwa walishindwa kuitumia hii fursa wakajikuta kwenye hayo matatizo makubwa ya kijamii na kiuchumi.
Nini maana yake?
Ili uweze kuzikabili changamoto na kuzitumia vizuri fursa zilizopo ni LAZIMA/SHARTI UJIANDAE. Lada niseme hivi maandalizi ni ya LAZIMA ili uweze kukabiliana na changamoto na kuzitumia fursa mbalimbali vizuri.
Zifuatazo ni njia kadhaa ambazo zitakusaidia kujiandaa kukabilina na changamoto zinazokuja mbele yako;
  • Kwa kuwa na malengo. Mithali 29:18.
  • Kwa kuomba bila kukata tamaa (ombeni msije mkaingia majaribuni).
  • Tafuta kujua kusudila Mungu katika maisha yako i.e kwa nini uliumbwa. Ukijua kusudi ni rahisi pia kujua mipango yake katika maisha yako.
  • Ukishajua nini wajibu wako hapa duniani, basi tekeleza kwa bidii, moyo na uvumilivu hayo majukumu. Ongeza ufahamu katika nyanja (field) yako ili upate maarifa ya kukusaidiauwe na ufanisi mzuri zaidi.
  • Kuwa makini na maisha yako (Zaburi 1:1). Hili litakujengea maisha ya nidhamu ili kuhakikisha unakaa kwenye mpango wa Mungu. Kuishi katika mpango wa Mungu kuna gharama zake. Gharama kubwa ni kujikana, ni lazima ujifunze na ukubali kuyahesabu mambo mengine kuwa hasara ili shauri la Kristo liweze kufanikiwa.
  • Weka ndani yako/tafakari neno/sheria ya Bwana usiku na mchana. Hii itakupa kuona njia ikupasayo kuiendea. “Neno la Bwana ni taa ya miguu yangu”.
  •  Jifunze kuwa na muda wa utulivu wa kuomba na kuwaza. Mungu huwa anasema katika utulivu. Utulivu wako ni fursa kwa Mungu kukufunulia FURSA za kukabiliana na changamoto unazozipitia na zinazokuja. 
Mungu akubariki, naamini ukiyaweka haya katika utendaji taratibu utaanza kuona fursa ambazo mungu anazileta kwako ili kukufanikisha. Kumbuka siku zote kwamba mawazo yake ni ya amani, kukupa tumanini siku zako za mwisho.
Nawapenda wale wanipendao na wanitafutao kwa bidii wataniona.
Neema ya Kristo iwe nawe.

UNAJIFUNZA NINI KUPITIA HUDUMA YA ANANIA NA BARNABA KWA PAULO?




UNAJIFUNZA NINI KUPITIA HUDUMA YA ANANIA NA BARNABA KWA PAULO?

 
Na; Patrick Samson Sanga.
Utangulizi;

Nakusalimu katika jina la Bwana, mpenzi msomaji.

Katika nyanja hii, leo nimeona ni vema tushirikishane kile ambacho Mungu alikifanya  kwa Paulo kupitia huduma ya Anania na Barnaba. Si watu wengi sana wanofahamu nafasi ya Barnaba na Anania kwa Paulo, kwanza mtu mwingine ukimuuliza unawafahamu kina Anania wangapi kwenye kitabu cha Matendo ya mitume wangekutajia Anania, mume wa Safira tu yule aliyeuawa kwa kuiba sadaka ya kiwanja na mkewe.

Nafasi ya Anania na Barnaba kwa Paulo.

Matendo ya Mitume 9: 10 -19 “kulikuwa na Mwanafunzi huko Dameski, jina lake aliitwa Anania……..
Matendo ya Mitume 9:27 inasema “ na Barnaba akamchukua—-‘

Watu wengi sana wanamfahamu vizuri Paulo na kumsifu kwa kazi nzuri aliyoifanya, hata mimi nuaungana na watu wenye mtazamo huo. Lakini si watu wengi pia wanaojua kwamba kazi aliyoifanya Paulo ni matunda ya uaminifu na utiifu wa Anania na Barnaba kwa Mungu wao. Watu wengi wanafikiri Paulo baada ya kuokoka tu, hapo hapo alianza huduma, si kweli wanatheolojia wansema inawezekana Paulo alikaa miaka 14 kwanza ndipo akaanza huduma. Na ukisoma vizuri kitabu cha wagalatia utagundua Paulo alikaa miaka 17 tangu kuokoka kwake na ndipo huduma yake ikapata kibali machoni pa mitume na watu wote.

Sasa katika kipindi hiki cha mpito licha ya kuendelea na huduma, Paulo alikuwa akifunzwa au akielekezwa kitu cha kufanya kupitia watu mbalimbali na hasa Anania na Barnaba. Anania ndio mwanafunzi wa kwanza aliyejenga msingi wa huduma ya Paulo, hii ina maana Anania angekosea huenda huduma ya Paulo ingesumbua pia.

Vivyo hivyo na Paulo alipokwenda Yerusalemu wanafunzi wote walimtenga. Barnaba ndiye aliyemchukua akamtia moyo na kumfariji na kisha akaitambulisha huduma yake kwa mitume na wanafunzi wengine na ndipo Paulo akapata kibali na uhuru wa kufanya huduma hiyo. Unaweza ukaona kama ni kitu kidogo lakini katika ulimwengu wa roho hawa watu waliweka alama kubwa sana na ndio maana hadi leo mimi na wewe tunabarikiwa na nyaraka za Paulo.

Jifunze yafuatayo kupitia ndugu hawa.

Moja, usiidharau nafasi yako mbele za Mungu, kumtumikia Mungu si mpaka usimame madhabahuni ufundishe maelfu ya watu. Wapo waliopewa kusimama madhabahuni lakini pia wapo waliopewa kutengeneza wale watakaosimama madhahuni. Using’ang’anie wajibu usiokuwa wa kwako. Kila mmoja katika mwili wa Kristo ana wajibu wake.

Paulo amejulikana sana lakini mbele za Mungu Anania na Barnaba wanaheshima zao kubwa zaidi kwa kukubali maagizo ya Mungu juu ya Paulo. Haijalishi watu wanaidharau kiasi gani huduma yako, uwe na uhakika Mungu anaithamini sana kazi yako. Huenda wanadamu wasikutukuze au kuona umuhimu, mchango wako katika ufalme wa Mungu bali uwe na uhakika pia Mungu ameiona na kuiheshimu sana kazi yako. Kwa Mungu Anania na Barnaba wana nafasi ya kwanza kuliko Paulo kwa sasbabu wao walikuwa walimu wa Paulo kiroho. Na neno linasema  mwanafunzi hampiti mwalimu wake.

Tekeleza wajibu wako na Bwana Mungu atakubariki katika hilo. Usitafute kuonenkana na watu, tambua kwamba Mungu yu pamoja na wewe. Siku zote zote lenga kutengeneza watu watakaotengeneza na kubadilisha maelefu ya watu. Usibakie kung’anga’nia madhabahu isiyo ya kwako kwa kugombana na wachungaji. Kama Mungu amekuletea hata mtu mmoja kama Anania, tekeleza wajibu wako vema kwa kumfunza huyo. Nani ajuaye huenda atakuwa mfano wa Paulo kwa kizazi cha leo. Sasa ni vema ukae kwenye nafasi yako na ndipo ufanisi wako utakuwa mzuri zaidi. Kadri unavyokuwa mwaminifu kwa huyo mmoja ndivyo Mungu atavyowapitisha na wengine wengi kwako upate kuwajenga na kuwafundisha njia ya Kristo ili waje kuwa watumishi wazuri wa kesho.

KIJANA ZINGATIA HILI, ILI UWEZE KULITUMIKIA KUSUDI LA MUNGU.




KIJANA ZINGATIA HILI, ILI UWEZE KULITUMIKIA KUSUDI LA MUNGU.

bible2 
“Huu ni waraka maalumu kwa vijana wote ambao bado hawajaoa au kuolewa”.
Na :  Sanga.P.S.

Kijana mwenzangu ninakusalimu kwa jina la Bwana. Katika mwezi huu nina neno fupi ambalo nimeona ni vema nikushirikishe na wewe juu ya ‘UMUHIMU WA KUUTAFAKARI MWISHO WAKO UKIUHUSIANISHA NA KUSUDI LA MUNGU JUU YAKO’

Tarehe 29/04/2008 nilifanya maombi maaulumu yaliyolenga kuombea vijana ambao bado hawajaoa au kuolewa, nikimsihi Mungu afungue milango ya wao kuoa au kuolewa, kwa sababu wengi wao ninaowasiliana nao bado hawajaoa au kuolewa.

Katika kunijibu Mungu alinipa mistari kadhaa na kunifunulia tafsiri yake, nami nikaandika kwenye kumbukumbu zangu na mwezi huu nimeona ni vema na wewe nikushirikishe mafunuo haya maana naamini yatakusaidia;   

Fungu la kwanza ni, Luka 19:41 – 44.
Soma fungu hili lote, mimi nitanukuu maneno machache tu. “Alipofika karibu aliuona mji, akaulilia, akasema, laiti ungalijua hata wewe, katika siku hii, yapasayo amani … siku zitakuja adui zako watakujengea boma … watakuangusha chini wewe na watoto wako … kwa sababu hukutambua  majira ya kujiwa kwako.

Fungu la pili ni, Isaya 1:2-3
“Sikieni enyi mbingu tega sikio ee nchi … kwa maana Bwana amenena; nimewalisha watoto na kuwalea nao  wameniasi, ng’ombe amjua Bwana wake, punda ajua kibanda cha Bwana wake, bali Israel hajui, watu wangu hawafikiri”.

Fungu la tatu (3) ni , Kumbukumbu  la Torati 39:29.
 “Laiti wangalikuwa na akili hata wakafahamu haya, ili watafakari mwisho wao”.

Katika mafungu haya matatu ya maandiko Roho mtakatifu alinifunulia yafuatayo;

*Kwanza alisema, usifikiri hao watu unaowaombea siwajibu. Wengi nilishawajibu, lakini wengine kwa sababu zao binafsi, wazazi wao, Viongozi wao n.k  hawajatii wazo langu juu yao/mapenzi yangu juu yao. Mimi ni Mungu ninayeangalia kesho/mwisho wa mtu/watu na lolote ninalofanya nimeliona mwisho wake. Sasa kwa kuwa hawa vijana wamekataa wazo langu kwa kutofikiria mwisho wao na kusudi langu kupitia wao na ndoa zao,  basi, hakika ndoa zao   zitakuwa na shida na baadhi yao wataniacha kabisa.

*Pili, Mungu kwa uchungu sana anataka mbingu na nchi zisikie na zijue kwamba   watoto wake ambao amewalisha na kulea  wamemuasi. Watoto hao wameshindwa kujifunza kupitia ng’ombe na punda, na tatizo lao ni kutokufikiri. Hii ina maana kutokufikiri kwao kumepelekea wao washindwe kumjua Mungu.  Kinamuuma sana Mungu, anapoona watu aliowaokoa na kuwafundisha au kuwaonyesha njia wapasayo kuiendea   wanakataa kwenda katika njia yake.

Zaburi 32:8 anasema “Nitakufundisha na kukuonyesha njia utakayoiendea, nitakushauri jicho langu likikutazama”. Sasa kitu kinachomuumiza ni pale anapowaonyesha watu njia yake au mapenzi yake kwao kuhusu wake/waume zao watarajiwa na akina nani halafu wao wanashindwa kutii. Licha ya kuwaonyesha au kuwajulisha mapenzi yake bado wameasi.


Ndugu kijana mwenzangu, natamani Mungu alete kitu hiki ndani yako kwa uzito ule ule aliouleta ndani yangu, ili usije ukakataa wazo la Mungu kwako na ukamkosea hata kuikosa mbingu kwa sababu tu ya mke au mume.

Sasa fanya yafuatayo ili kukaa katika mapenzi yake;

(a)   Jifunze kutafakari mwisho wako, ukijua ya kwamba mwisho wako uko mikononi mwa Mungu. Na kwa sababu hiyo maamuzi yoyote unayoyafanya ni lazima,  na si ombi umruhusu Mungu akuongoze ili uenende katika njia zake.
(b)   Haijalishi kwa jinsi ya mwili huyo mtu ana upugnufu/udhaifu wa aina gani kwa mtazamo wako, maadam una uhakika ni mtu wa mapenzi ya Mungu uishi naye, basi usijaribu kukataa huyo mtu kwa sababu Mungu ameona unakokwenda kukoje na huyo aliyemleta ndiye ambaye mtafika naye mwisho wenu.  
(c)    Hivyo basi wazo lolote/kijana/mtu yoyote anapokuja kwako kutaka   muoane na ndani yako unaona hakika ni mtu wa mapenzi ya Mungu, basi  kabla hujakataa kwa sababu zako binafsi, kaa chini utafakari, mhoji Mungu kwa maswali yanayokutatiza. Unapokwenda mbele za Mungu siku zote yeye ni mwaminifu atakupa majibu ya msingi na nina kuhakikishia unapotii uongozi wa Mungu kuna baraka za ajabu sana. Lakini unaposhindwa kutii  itakugharimu kuliko unavyofikiri.

  *Mungu anapokuonyesha/anapokupa mke au mme hamleti kwako kwa lengo la kukukomoa, bali anakua ameangalia kwanza kusudi lake, changamoto zilizopo mbele yenu na umbali mnaotakiwa kusafiri kwa pamoja kisha ndio anawaunganisha kwa kukupa mtu (mke au mume) ambaye anajua ukiwa naye hakika kusudi lake litafikiwa na mtaweza kuzikabili na kuzishinda changamoto zote zitakazojitokeza.

Hivyo mwenzi yoyote unayempata kama una hakika katoka kwa Mungu hata kama ana mapungufu gani kwa fikra zako au wazazi au dhehebu lako mimi nakushauri usimkatae, kwa sababu kwa huyo wewe utaweza kulitumikia shauri la Bwana.

Aliye na masikio na asikie lile ambalo Roho wa Bwana asema na vijana.

NINI MATARAJIO YA MUNGU KWA VIJANA?

                                      NINI MATARAJIO YA MUNGU KWA VIJANA?
A
Na: Patrick Samson Sanga.
 1yohana 2:14 “…. Nimewaandikia ninyi,vijana kwa sababu mna nguvu,na neno la Mungu linakaa ndani yenu ,nanyi mmeshinda yule mwovu.”Mungu anao mtazamo wake binafsi juu ya kila kundi la watu chini ya jua,.Na kila kundi mfano wa wamama,wajane,watoto,vijana kuna mambo fulani ambayo Mungu anatarajia kila kundi litatekekleza. Mungu anazungumza na vijana na kusema nimewaandikia ninyi vijana kwa sababu moja mna nguvu,mbili neno la Mungu linakaa ndani yenu, na tatu mmemshinda yule mwovu.
Nguvu zinazozungumziwa hapa ni nguvu,uweza wa Mungu wa kukusaidia kutekeleza maagizo yake. Na kwa sababu hiyo basi kuna matarajio ya Mungu kwa hao vijana. Sasa lengo la ujumbe huu mfupi ni kukueleza nini Mungu anatarajia/anategemea kwamba utafanya sawasawa na nafasi aliyokupa mbele zake na uwezo aliokupa. Matarajio ya Mungu kwa vijana ni kama ifuatavyo:
*Moja, Vijana wauteke ufalme wake.
Mathayo 11:12 “Tangu siku za Yohana mbatizaji hata sasa ufalme wa mbinguni hupatikana kwa nguvu,nao wenye nguvu wauteka”. Biblia inapozungumzia ufalme wa Mungu inazungumzia habari za utawala wa Mungu . Hivyo ni matarajio ya Mungu kwamba popote pale vijana walipo basi watatengeneza mzazingira ya Mungu kutawala katika maeneno waliyopo iwe darasani, Chuoni, Kazini, Kanisani nk na hii ni kwa sababu wana nguvu.Sikiliza vijana wana nguvu na ufalme unapatikana kwa nguvu,maana yake Mungu anatarajia vijana watumie nguvu zao kuuteka ufalme wake na kuurusu uchukue utawala duniani.
*Mbili,Vijana warejeshe urithi na mali za wana wa Mungu zilizotekwa.
Mwanzo 14:13-16. “…Akawapa silaha vijana wake,walozaliwa katika nyumba yake,watu mia tatu na kumi na nane,akawafuata mpaka Dani”. Hizi ni habari za Ibrahamu aliyeenda kumuokoa nduguye Lutu baada ya kuwa ametekwa.Ili kurejesha urithi wao na mali zao ilimbidi Ibrahimu atumie nguvu kazi ya vijana. Na hivyo hata leo Mungu anatarajia kwamba vijana wasimame kwenye nafasi zao na kupambana kwa ajili ya afya,ulinzi, uchumi,uponyaji,mafanikio ya watu wake. Hebu jipe dakika moja halafu tazama jinsi shetani anavyotesa watu na kudhulumu afya zao, ujana wao, ndoa zao ,uchumi wao nk.Ni nani watakaorejesha hali nzuri, urithi huu kwa wana wa Mungu , ni Mungu kupitia Vijana.
*Tatu, Vijana wasikosee katika kufanya maamuzi ya kuoa au kuolewa.
Mithali 5:18 “Chemichemi yako ibarikiwe;nawe umfurahie mke wa ujana wako”.Sikiliza Mungu anataka ndoa yako iwe ni ndoa ya mafanikio na ya furaha, maana yake ni ndoa ambayo hautaijutia kwamba kwa nini nilimuoa au kuolewa na huyu mtu.Sasa ili ndoa yako iwe ni ya furaha na amani, ni lazima huyo mwenzi wako umpate kwa uongozi wa Mungu mwenyewe. Sasa mtazamo wa Mungu kwa vijana ni huu vijana hawatakosea kufanya haya maamuzi kwa sababu tayari Neno la Kristo limejaa kwa wingi ndani yao.Kumbuka neno la Kristo ni taa ya miguu yangu.
*Nne, vijana wawe wasuluhishi wa matatizo katika jamii na taifa.
 Mithali 1:4 “Kuwapa wajinga werevu,na kijana maarifa na hadhari”. Leo ndani ya kanisa, jamii tunayoishi na katika taifa kwa ujumla yapo matatizo mbalimbali ya kiroho,kiuchumi,kijamii,kiafya,kimwili,kibiashara,kindoa nk. Sasa Mungu anatarajia vijana ndio watumike kusuluhisha matatizo haya mbalimbali katika jamii kwa sababu ya wingi wa neno la Kristo ndani yao. Hii ina maana mtu mwenye neno la Kristo kwa wingi ndani yake basi maana yake ana upeo mkubwa wa kuelewa mipango na njia za Mungu za kuwatoa watu wake kwenye matatizo yanayowakabili. Hivyo tumia fursa hiyo kutatua matatizo hayo na kusuluhisha kwa sababu ya Kujua mawazo na njia za Mungu za kuwatoa watu wake kwenye shida walizonazo.
*Tano, vijana walitumikie kusudi lake la kuhubiri habari njema.
 Mathayo 28:19 “Basi enendeni mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi,mkiwabatiza kwa jina la baba na la mwana na la Roho Mtakatifu”. Sikiliza kwa sababu ya nguvu ambayo Mungu amewekeza kwa vijana basi ni matarajio yake kwamba wewe kama kijana utatumika kuwaeleza watu wengine habari njema za Yesu Kristo ziletazo amani. Ni matarajio yake kwamba vijana watapita nyumba kwa nyumba , mtaa hadi mtaa wawaambie wengine kuhusu huyu Yesu, wakiwafungua waliofungwa na kuutangaza mwaka wa Bwana uliokubalika. Naamini haya matarajio matano ya Mungu kwako kama kijana mwenzangu basi yatakusaidi sasa kukaa kwenye nafasi yako ili Mungu ajivunie kuwa na kijana kma wewe.
Amani ya Kristo na iwe pamoja nanyi.

KWA NINI VIJANA WENGI HAWAJAKA KWENYE NAFASI ZAO KI-MUNGU?




KWA NINI VIJANA WENGI HAWAJAKA KWENYE NAFASI ZAO KI-MUNGU?

Na : Patrick Sanga.

Iyohana 2:14

 Kila kundi katika kanisa, jamii na hata nchi Mungu amelipa nafasi na wajibu wake maalumu wa kutekeleza. Pia Mungu anao mtazamo wake binafsi na matarajio yake kwa hayo  makundi
mbali mbali ndani ya nchi. Vijana, watoto, wababa, wazee, wanawake, viongozi wote / yote yana mtazamo wake mbele za Mungu. Ukimuuliza Mungu  nini mtazamo  wako  kwa vijana, atakujibu  soma vizuri IYohana 2:14 maana  yake Mungu anawatazama vijana kama watu wenye nguvu, watu ambao neno la Mungu linakaa ndani yao na pia wamemshinda mwovu.
 Sasa  ukirudi  mazingira  halisi unaona kwa  asilimia kubwa vijana wengi hawako kwenye nafasi ambazo Mungu aliwakusudia. Lengo la somo hili ni :--         Kueleza sababu za kwa nini  vijana wengi hawajakaa  katika nafasi zao.-         Kumweleza kijana mambo ya kujiepusha nayo ili  aweze kukaa kwenye nafasi yake.-         Kumpa kijana maarifa yatakayomsaidia kurejea kwenye nafasi yake na ili aweze kutekeleza matarajio ya Mungu kwake. Zaidi ujumbe huu umekusudia kulenga na kuelewesha vijana waliokoka, nazungumza  na vijana waliookoka maana hawa ndio ambao Mungu amewatamkia maneno haya au kuwa namtazamo huu juu yao. Zipo sababu  nyingi lakini hizi zifuatazo ni za msingi na zimesababisha wengi kuishi maisha nje ya kusudi la Mungu na kufa bila kutekeleza matarajio ya Mungu  kwao sababu hizo ni:-
-         Moja vijana wengi hawajajazwa nguvu za Roho Mtakatifu.
 Biblia inasema katika matendo ya Mitume 1:8 kwamba “lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajia  juu yenu Roho  Mtakatifu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika  Yerusalemu, na katika uyahudi wote, na samaria, na hata mwisho wa nchi”. Hivyo vijana wengi hawajakaa katika nafasi zao  kwasababu wengi wa vijana leo makanisani  hawajajazwa nguvu za Roho Mtakatifu si kwamba  Mungu hataki kuwajaza lakini shida ipo kwa vijana wenyewe wengine kutotaka kujazwa nguvu hizo, lakini wengine hawajui nini wafanye wajazwe  nguvu za Roho  Mtakatifu  na wengine wanajua lakini hawana kiu ya kujazwa nguvu hizo.
         Pili vijana wengi hawajui namna ya kuenenda kwa Roho .
Paulo kwa warumi anasema” kwa kuwa wote wanaoongozwa na Roho wa Mungu, hao ndio wana wa Mungu” Warumi 8:14 na pia kwa wagatia  anasema” Basi nasema  enendeni kwa Roho hamtatimiza kamwe   tamaa za mwili “Gal 5:16.         Kuna  wengi waliojazwa lakini si wote wanaoenenda au wanaoishi wa Roho. Vijana wengi Mungu amewapa  vitu vizuri  sana ndani yao lakini kwa sababu ya kukosa utiifu na kutoenenda kwa  Roho wameshindwa kusimama kwenye nafasi zao.    
Tatu  vijana wengi wameshindwa kushirikiana  na upako wa Mungu uliodhihirishwa kwao.
Hili ni tatizo kubwa kwa  kweli, Mara nyingi Mungu  amekuwa akiwapa upako, nguvu au uweza wa kufanya mambo  mbalimbali vijana. Sasa si vijana wote  wanaojua  namna  ya kushirikiana  na  huo upako ambao Mungu aliwapa kwa jambo fulani  Mfano, Mungu anaweza akampa kijana upako wa kuomba lakini  kijana  huyo badala ya kuomba yeye anaangalia  mpira, au ni mwanafunzi anatakiwa kusoma na Mungu ameleta upako  huo  sasa yeye anaenda kuomba mambo huwa hayakai hivyo. Upako lazima utumike kwa kusudi  lile  uliotumiwa. Upako wowote unaokuja kwako unakuja kwa kusudi maalumu. 
Nne Kukosa maarifa ya Mungu.
Mungu anasema katika Hosea 4:6 kila kipengele cha kwanza  watu wangu wanaangamia kwa kukosa maarifa na pia katika Zaburi 119:9 anasema “Jinsi gani kijana aisafishe njia yake? Kwa kutii akilifuata neno lake”. Sasa kwa sababu  nazungumza na vijana naweza nikaweka mistari huu hivi “Vijana wangu wanaagamizwa kwa kukosa maarifa. Maarifa yanayozungumzia hapa ni mafundisho ya neno la Mungu.
Vijana wengi wako  tayari kuangalia mechi mbili mfululizo kuanzia saa nne kasoro usiku hadi saa  nane kwa masaa ya Kitanzania, lakini hawako tayari kusoma Biblia kwa saa moja, wako tayari kuangalia “Movie” za kinigeria, au za kizungu hata masaa matatu (3) lakini si kuangalia na kusikiliza mafundisho ya Neno la Mungu. Na Biblia inasema Apendaye mafundisho hupenda maarifa. Sasa kwa vile vijana wengi hawapendi mafundisho ndiyo maana hawako kwenye kusudi la Mungu. 
Tano, vijana wengi bado wanaipenda dunia,
Mzee Yohana katika 1Yohana 2:15” Msiipende dunia, wala mambo yaliyomo katika dunia, mtu akiipena dunia kumpenda Baba  hakupo ndani yake”. Na pia  Daudi anasema katika Zaburi  1:1 Heri mtu yule asiyekwenda katika shauri la wasio haki wala  kusimama katika njia ya wakosaji wala     hakuketi barazani pa wenye mzaha.Ni vijana wachache sana katika  kanisa la leo ambao wako tayari kujikana nafsi zao kwa ajili ya Mungu wengi wanapenda kupoteza muda kwa habari  zisizo za Msingi, wengi wanapenda mzaha na utani, ni vijana wachache  ambao wanaweza kuacha kuangalia mchezo kwenye TV, au  akakataa kwenda kutembea ufukweni kwa lengo  la kuomba, au kusoma Neno, ninachojaribu kusema hapa ni hiki, najua kila jambo lina wakati wake, lakini ni vijana wachache sana waliojizuia katika mambo ya mwili kwa ajili ya kufanya yaliyo mapenzi ya Mungu.
Sita, Vijana wengi hawajazivaa silaha za vita.
 Waefeso 6:11 Vaeni Silaha zote za Mungu, mpate kuzipinga hila  za shetani.Viajana wengi wameshindwa kumshinda mwovu kwa sababu hawazajivaa silaha za vita. Wengine hawajui silaha za vita ni zipi? Lakini wengine wanajua lakini hawajazivaa. Ile sura ya sita ya waefeso 6:10-18 Paulo anazungumzia silaha za vita, ambazo ni kwlei, haki, amani, Imani, wokovu na Neno la Mungu. Sasa hizi ni silaha na kama ni silaha zina namna zinavyovaliwa na namna zinavyotumika. Sasa si vijana wote waliozivaa silaha, wengi hawasomi neno la Mungu, hawatendi haki, wengi wana imani ya maneno isiyo ya  Matendo.
Saba, Vijana wengi wanaishi bila kuwa na malengo katika maisha yao / maono.
Mithali 29:18. Inasema “Pasipo maono watu huacha kujizuia bali ana heri mtu yule aishikaye sheria”. Hivi leo  ukiwauliza vijana wengi kwamba una maono au hasa malengo gani katika maisha yako? Asilimia kubwa watakujibu  sina malengo  yeyote  yale.Wakati huo huo hakuna aliyeumbwa kwa bahati mbaya Yeremia  29 :12. Kwa kila mtu Mungu analokusudi maalum la kumuumba na pia anayo malengo na mikakati ya kumpa huyu mtu atekeleze katika maisha yake. Sasa kwa sababu vijana wengi  hawana na hawajajua  hayo malengo ndio maana wanafanya  kila kinachotokea mbele yao bila kujua  kama ni kusudi la Mungu.
    Naamini  baada ya kuwa umesoma ujumbe huu umepata maarifa ya kukusaidia kukaa katika nafasi yako kama kijana kwa sababu umeshajua sababu za kuktokukaa kwenye nafasi yako.

Friday, April 20, 2012

IJUE NA KUITUMIA NAFASI YAKO KAMA MLINZI KWENYE ULIMWENGU WA ROHO (Part 3)



IJUE NA KUITUMIA NAFASI YAKO KAMA MLINZI KWENYE ULIMWENGU WA ROHO (Part 3)

(Umuhimu wa taarifa na mahusiano mazuri baina ya mlinzi na watu wa eneo lake)
Na: Patrick Sanga
Katika sehemu ya pili naliahidi kwamba ningeanza kuelezea kuhusu nafasi mbalimbali za ulinzi, lakini ndani yangu nimesikia kuandika mambo kadhaa yafuatayo tena kabla sijaanza kuandika kwa habari ya nafasi husika. Ni imani yangu kwamba sehemu ya nne itaanza kwa kuelezea nafasi husika, fuatana nami tuendeleae.
Jambo ambalo nimesukumwa niandike kwa habari ya eneo hili la tatu ni umuhimu wa taarifa na mahusiano mazuri baina ya mlinzi na watu wa eneo lake.
Jambo la kwaza – Umuhimu wa taarifa ya mlinzi kwa watu wa eneo lake
Hebu tuangalie jambo hili kupitia kitabu cha Mathayo 25:1-13. Hii ni habari ya wanawali kumi waliokuwa wakimsubiri Bwana Harusi. Biblia inatuambia watano kati yao walikuwa na busara na watano walikuwa wapumbavu. Busara ya wale watano wa kwanza ni kuwa na taa zenye mafuta ya akiba huku wakimsubiri Bwana, na upumbavu wa wale watano wengine ni kuwa na taa zisizo na mafuta ya akiba huku wakimngoja Bwana harusi pia.
Kwa sababu ya Bwana harusi kuchelewa wanawali hawa wote waliamua kulala. Ule mstari wa sita na saba inasema ‘Lakini usiku wa manane, pakawa na kelele, Haya, Bwana arusi; tokeni mwende kumlaki. Mara wakaondoka wanawali wale wote, wakazitengeneza taa zao’.
Katika sehemu ya pili ya somo hili niliandika kwamba jifunze kuitazama taarifa ya mlinzi kama fursa ya matengenezo. Biblia iko wazi kwamba wanawali hawa waliamua kulala baada ya kuona Bwana harusi wao amechelewa. Kumbuka kwamba lengo la wote hawa ilikuwa ni kumlaki Bwana Harusi. Sasa kilichowaamsha toka usingizini ni ‘kelele za taarifa’ ambazo ninaamini zilikuwa za walinzi ambao jukumu lao ilikuwa ni kutoa taarifa juu ya uwepo au ujio wa Bwana harusi husika.
Kutokana na mfano huu tunajifunza kwamba mosi taarifa ya mlinzi/walinzi iliwasaidia wanawali kuamka kutoka usingizini maana walikuwa wamelala. Licha ya taarifa kuwasiaida kuamka usingizini, taarifa ya mlinzi ilitoa fursa ya wanawali kujiandaa. Tumeona katika mstari wa saba kwamba punde baada ya taarifa wale wanawali wakaamka na kuziandaa/zitengeneza taa zao. Naam taarifa ya walinzi ilitoa fursa ya matengenezo. Hivyo hata sasa Mungu anapoleta taarifa kwako, ujue analeta taarifa ya matengenezo, naam mbele kuna jambo linakuja, hivyo analeta taarifa mapema kupitia walinzi wako au wa eneo lako ili uitumie kutenda yapasayo. 
Jambo la pili – Umuhimu wa kuwa na mahusiano mazuri kati ya Mlinzi na watu wa eneo lake.
Kupitia mfano huu wa wanawali kumi tunagundua pia kwamba, taarifa ya mlinzi ilitoa fursa ya mawasiliano baina yao. Kabla ya taarifa hatuoni wanawali hawa wakiwasiliana kwa jambo lolote. Si hivyo bali pia tunagundua kwamba baada ya taarifa ya mlinzi ndipo fahamu za wale wanawali wapumbavu zikafunguka na wakajua mafuta yao hayatoshelezi. Kwa mujibu wa Biblia harusini aliruhusiwa kuingia mtu (mwanamwali) mwenye taa inayowaka yaani taa yenye mafuta.
Je, ni kwa nini wale wanawali wapumbavu kabla hawajaenda kulala hawakufikiri kwamba mafuta haya yakiisha na hatuna ya akiba hatuwezi kuingia harusini?  Huenda hawakujua kwamba mwanamwali mwenye taa inayowaka ndiye atakayeruhusiwa kuingia harusini. Jambo ninalotaka ulione ni kwamba pamoja na kutokujua kwao, walinzi wa mji walijua nini kinatakiwa kwa mtu kuingia harusini. Laiti wanawali wangekuwa na mahusiano mazuri na walinzi wa mji wangepewa siri kuhusu ujio wa Bwana harusi wao. Lakini kwa sababu hawakuwa na mahusiano mazuri na walinzi, walishindwa kuwauliza wale walinzi mahitaji ya msingi atakapokuaja Bwana harusi. Naam wakajikuta wameachwa na Bwana wao walipoenda kutafuta mafuta. 
Ukweli huu kuhusu mahusiano unathibitishwa katika kitabu cha Wimbo Ulio Bora 3:3 unaosema ‘Walinzi wazungukao mjini waliniona; Je! Mmemwona mpendwa wa nafsi yangu’. Habari hii inatueleza habari za kijana aliyekuwa anamtafuta mwenza (mpenzi) wake kwa muda mrefu bila mafanikio. Katika kuendelea kumtafuta ndipo akakutana na walinzi wa mji, akawauliza mmemwona mpendwa wa nafsi yangu?          Ni imani yangu walinzi wale walimjibu, kwa sababu mstari wa nne unatumabia ‘kitambo kidogo tu nikishakuwaondokea, nikamwona mpendwa wa nafsi yangu, Nikamshika nisimwache tena…’ Hivyo ufumbuzi wa tatizo (hitaji) la huyu kijana ulipatikana kwa walinzi wa mji. Kwa hakika mahusiano mazuri ya Walinzi na yule kijana yalipelekea hitaji la kijana kufanikiwa au kufikiwa.
Kutokana na habari hii ni dhahiri kwamba walinzi wamewekwa kwenye nafasi zao ili kuleta ufumbuzi juu ya changamoto zinazomkabili mwanadamu kwa kumjulisha mawazo ya Mungu juu yake, ili pia kumsaidia mwanandamu aishi kwa kulitumikia shauri la Mungu katika siku zake. Biblia katika kitabu cha Isaya 62:6-7 inasema  ‘Nimeweka walinzi juu ya kuta zako, Eee Yerusalemu; hawatanyamaza mchana wala usiku; ninyi wenye kumkumbusha BWANA, msiwe na kimya; wala msimwache akae kimya, mpaka atakapoufanya imara Yerusalemu, na kuufanya kuwa sifa duniani’.
Mungu anataka yawepo mawasiliano na mahusiano mazuri kati ya Mlinzi (Walinzi) na wanaolindwa. Katika andiko hilo hapo juu, licha ya Mungu kuweka walinzi juu ya kuta za Yerusalemu ilibidi awape taarifa na wakazi wa mji huo, ili wasije, walinzi hao wakatoa taarifa ya kile Mungu amesema na wakazi wa Yesrusalemu wakapuuza, mwisho wao wakaangamia.
Ukisoma pia Biblia katika kitabu cha Mathayo 24:43 inasema ‘Lakini fahamuni neno hili; kama mwenye nyumba angalijua ile zamu mwivi atakayokuja, anagalikesha, wala asingeliacha nyumba yake kuvunjwa’. Naam kiroho milinzi au walinzi ndio waliopewa uwezo wa kuona nini kinakuja juu yako, ndoa yako, kazi yako, huduma yako, taifa lako nk. Kwa sababu hii ni muhimu sana kuwa na mahusiano mazuri na mlinzi au walinzi ambao Bwana Mungu amekuweka chini ya Mlango au Himaya yao. Naam kufanikiwa kwa kazi ya mlinzi katika nafasi yake kunategemea mahusiano na ushirikiano anaopata kutoka kwa watu wa eneo lake.   
Mungu akubariki kwa kufuatilia mfululizo huu, usiache kuombea muendelezo wa somo hili. Tutaendelea na sehemu ya nne…