Friday, April 20, 2012

NAJUTA KWA NINI NILIKUBALI KUOLEWA?



NAJUTA KWA NINI NILIKUBALI KUOLEWA?

Na: Patrick Sanga
Baada ya mwaka mmoja wa ndoa, Merian asema anajuta kwa nini alikubali kuolewa. Merian na Joseph (haya siyo majina yao halisi) ni mtu na mumewe. Nikiwa katika Mkoa wao kikazi, niliamua kuwatembela wanandoa hawa. Merian alinipokea na kunikaribisha ndani kwa furaha sana. Tukaanza kuongea nami nikamuuliza, Joseph yupo? Akaniambia bado hajarudi kutoka kazini, hata hivyo kaniambia yupo njiani anakuja.
Tukaanza kuzungumuza mambo kadha wa kadha na kisha nikamuuliza mnaendeleaje na ndoa yenu changa? Baada ya kuwa nimemuliza swali hili akacheka na kisha akaanza kwa kusema, nyie maisha haya ya ndoa yaacheni tu, kwa kweli najuta kwa nini nilikubali kuolewa? Kauli hii ilinishtua sana kwa sababu kwanza sikuitegemea na pia ndoa hii ilikuwa ndio imetoka kutimiza mwaka  wa kwanza tu.
Kwa haraka kabla hajaendelea nikamzuia asiseme hayo maneno tena, maana nilijua kadri anavyosema ndivyo anavyozidi kuumba uharibifu kwenye ndoa yake. Akaniambia usinizuie, si umeuliza tunaendeleaje, subiri nimalize kukuelezea. Ndipo akaanza kuniambia kile kilichompelekea kusema anajuta kwa nini alikubali kuolewa (Kwa ufupi ni changamoto ambazo kwa ujumla naweza kusema za kawaida, hata hivyo sitaweza kuziandika hapa kwa sababu maalum).
Katika maelezo yake Merian aliniambia, vijana wengi sana walinifuata ili kunioa, mie nikawakataa, natamani ningeolewa na yoyote kati ya wale wengine, lakini si hapa nilipo na laiti likitokea lolote sasa (kwa maana ya mwenzake kufa) sitakubali kuolewa tena.
Mpenzi msomaji sijui kama unakiona ninachokushirikisha kupitia maisha ya wanandoa wenzetu hawa. Kumbuka ni mwaka mmoja tu wa ndoa, na leo tunashuhudia Merian akijutia maamuzi yake ya kuolewa na Joseph. Licha ya kwamba ni mwaka wa kwanza tu, lakini wawili hawa wameokoka pia.
Maelezo ya dada Merian yaliniletea maswali matano (5) ndani yangu ambayo ndiyo ninayotaka tujifunze kutoka kwake;
Swali la kwanza; Je! Merian, alijua nini maana ya ndoa kabla ya kuolewa?
Swali la pili: Je, Merian alijua aina ya maamuzi anayotaka kufanya kabla ya kuolewa?
Swali la tatu: Je, Merian alimuhusisha Mungu kabla ya kuolewa ili ampate mwenzi sahihi wa kuishi naye?
Swali la nne: Je, Merian alikuwa amejiandaa/andaliwa kifikra kuishi kama mke?
Swali la tano: Je, mpaka sasa, Merian anajua wajibu wake ni nini kwenye ndoa?
Kutokana na maswali haya niliwaza mambo matatu ambayo, nafikiri kama vijana wangefahamu yatawasaidia katika ndoa zao;
  • Moja, ni vema vijana wajifunze kumshirikisha Mungu awaongoze kupata mwenzi sahihi wa maisha, kabla hawajaingia kwenye hizo ndoa. 
  • Mbili, ni vema vijana wakajifunza kufikiri kimapana kabla ya kuingia kwenye ndoa. Swali la msingi katika kufungua tafakuri hii, ni kwa nini mtu aoe au kuolewa? Ni swali fupi lakini kama wewe ni mtu ambaye hufikiri kimapana swali hili litakujengea msingi mzuri wa baadaye. Naam kile kitabu cha 1 Wakorinto sura nzima ya saba kikuongoze katika tafakuri hii.
  • Tatu, ni vema vijana wangefunzwa/kuandaliwa vya kutosha kuhusu ndoa na hasa wajibu uliopo mbele yao. Endapo kama Serikali inawasomesha watumishi wake kwa lengo la kuwaongezea uwezo na maarifa ya kutekeleza majukumu yao, basi ifike mahali kanisa, wazazi, viongozi wa vijana nk makundi haya yaone umuhimu wa kuwaandaa vijana wao kuyakabili maisha ya ndoa.
Watu wengi hufikiri chanzo cha matatizo kwenye ndoa zao ni Shetani. Ndio hii ni sababu moja, lakini sababu nyingine kubwa, ni watu wengi kukosa ufahamu wa masuala ya ndoa kabla na baada ya kuingia kwenye hizo ndoa. Naam wakati watu wanasema Shetani anaangamiza ndoa zetu, Mungu anasema, ndoa za watoto wangu zinaangamizwa kwa kukosa maarifa (Hosea 4:6).
Ni imani yangu kwamba, kama mambo haya yatazingatiwa, sehemu kubwa ya changamoto ambazo wanandoa wanapitia, zingepata ufumbuzi wa haraka. Natoa wito kwa wadau mbalimbali wa masuala ya ndoa na hasa Wachungaji, Walimu na Viongozi wa makundi ya kiroho, kuanzisha utaratibu wa kuwa na mafunzo maalum kuhusu ndoa, kwa vijana ambao wameweka wazi dhamira zao za kuingia kwenye maisha ya ndoa.
Ni vema pia, hata kwa wale ambao wako ndani ya ndoa, wakawekewa utaratibu wa kuwa na mafunzo ya mara kwa mara, maana kwa mtazamo wangu ndoa ni shule ambayo, wahusika wanapaswa kuongeza (kujifunza) ufahamu wao kila siku, ili kulitumikia vema kusudi la Mungu. 
Bwana Yesu na utusaidie watoto wako, Amen!

UPONYAJI WA NDOA ZETU



                        UPONYAJI WA NDOA ZETU

 Na: Patrick Sanga
 

Siku moja mama Allen (hili siyo jina lake halisi) alianza kunishirikisha mambo ya ndoa yake yanavyomtesa. Akaniambia mwanangu hizi ndoa tunapenda tu kuingia bila kujua kilichomo ndani yake. Hivi unavyoniona sina hamu kabisa ya ndoa, maana maisha tunayoishi (ingawa kwa nje watu wanaona tuko pamoja), lakini ukweli ni maisha ya taabu na majuto karibu kila siku.
Tabia ya mume wangu imefika mahali haivumiliki. Nikamuuliza tatizo ni nini hasa? Akasema ni fedha, elimu yake na kutoka nje ya ndoa. Fedha ya mume wangu wanaijua wazazi wake na si wazazi wangu, kwani mara kwa mara yeye hutuma fedha kwa wazazi wake. Inaniuma maana natamani hata mie  wazazi wangu niwatumie fedha pia.
 Mume wangu ni kweli Mungu kamjalia kuwa na elimu ya kutosha, lakini elimu yake imekuwa dharau kwangu nisiye ana elimu kama yake. Maana hunisema kwa sababu ya elimu yangu ndogo, kazi yangu na mshahara wangu mdogo ukilinganisha na wake.  Kubwa na baya Baba Allen sio mwaminifu katika ndoa, sina amani na hasa ukizingatia ugonjwa huu wa ukimwi, nina mashaka makubwa sana ndani yangu.
Nikamuuliza umefanya jitihada gani ili kutafuta ufumbuzi wa changamoto hizi za ndoa yako? Akajibu akasema nimeamua kuishi naye kwa kuzikubali tofauti zetu (agree to differ). Kwa lugha nyingine nimekubali kuishi na hali hii, kwamba haya ndiyo maisha yangu ya ndoa chini ya jua. Hivyo imefika mahali sina jingine la kufanya ila kukubali kwamba mwenzangu yuko vile na mimi niko hivi, tutendelea kuishi kwa kutofautina hadi kifi kitutenganishe, kwani jitihada za kujaribu kurekebisha mambo haya zimekwama.
Baada ya kusikia maelezo haya niliumia sana, nikamshauri mambo kadhaa ya kufanya ili kuiponya ndoa yake. Lengo langu la msingi katika kuandika habari za mama Allen ni kujaribu kukufukirisha mwanandoa mwenzangu mambo kadhaa yatakayokusaidia kuiponya ndoa yako pia;
  • Jambo la kwanza – Ndoa ni wito wa upungufu na hivyo suala la uvumilivu ni la lazima.
Si watu wengi wanaojua kwamba ndoa ni wito wa mapungufu pia. Maandiko yanasema ‘ Kwa hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja’ (Mwanzo 2:24).
Ni dhahiri kwamba watu wanapooana wanakuwa wametoka katika asili na malezi (background) tofauti hasa kutokana na mazingira waliyokulia. Ile tu kwamba huyu anatoka katika familia hii na huyu ile, fahamu kwamba lazima kutakuwa na tofauti kadhaa katika ndoa hiyo. Naam tofauti zenu ndiyo sehemu ya  mapungufu kwenu kama  wanandoa. kwa sababu wewe ungependa mwenzako awe hivi na yeye kuna vitu ambavyo angependa vibadilike kwako.
Na wala usije ukajiona wewe upo kamili, naam kwa upande wako unaweza kuwa sawa lakini kwa mwenzako, hauko kamili. Ni vizuri ukafahamu kwamba unapoingia kwenye ndoa, utakabilana na mapungufu ya mwenzi wako. Kwa sababu hii suala la uvumilivu, kuchukuliana, kusameheana kwa wanandoa ni la msingi ili kufikia mahala pa kutengeneza tabia au mfumo mpya wa ndoa yenu.
  • Jambo la pili – Haijalishi mwenzi wako anatabia mbaya kiasi gani, Yesu anaweza kumbadilisha.
Jambo la pili ambalo nimeoana vema kusisitiza ni kwamba wewe mama au baba ambaye ndoa yako ipo kwenye misukosuko kama ya mama Allen pengine na kuzidi, usifike mahala pa kukata tamaa na kuamua kuishi kwa kuzikubali tofauti zenu kama sehemu ya maisha. Kwa kufanya hivyo utakuwa unamzuia Roho Mtakatifu kukusaidia kuiponya ndoa yako. Ni lazima kwanza ubadili fikra zako na mtazamo wako kwamba, kwa Mungu hakuna lisilowezekana na hivyo haya si maisha yangu ya ndoa ninayostahili kuyaishi.
Kwa Mungu sisi tu watoto wake. Hakuna Baba mwenye kufurahia kuona maisha ya ndoa ya watoto wake yanakuwa ya majuto. Mungu alipoleta wazo la ndoa ilikuwa ni kwa ajili ya kusudi la ufalme wake na kuwa furaha kwa watoto wake na si majuto. Nasikitika kusema leo, ndoa nyingi zimekuwa ni majuto na si kile Mungu alikiona wakati wa uumbaji hata akasema, kila kitu nilichokifanya ni chema sana (Mwanzo 1:31).
Kwa kilio kilichopo kwenye ndoa hivi sasa ni dhahiri kwamba kuna mahali kama wanandoa tumekosea na kumpa Iblisi nafasi (Waefeso 4:27) hata ameleta majuto kiasi hiki. Ushauri wangu ni kwamba ni vema kila mwanandoa akasimama kwenye nafasi zake (Mwanaume kama kichwa na Mwanamke kama Mlinzi na Msaidizi nk) kwa pamoja tumpinge Shetani naye atatukimbia. Endapo mwenzi wako hayuko tayari kwa hili au hamjui Mungu wako, basi wewe mwenye kujua siri hii kama anza, maana kwa Mungu mtu mmoja natosha kuleta uponyaji wa Taifa, je si zaidi ndoa yako? Naam usikate tamaa, Mungu wetu, ni MUNGU ASYESHINDWA.

Bwana Mungu na akusaidie katika kuzikabili changamoto za ndoa yako.

UHURU WAKO KATIKA KUMTUMIKIA MUNGU, UNATEGEMEA UHUSIANO WAKO NA MWENZI WAKO



UHURU WAKO KATIKA KUMTUMIKIA MUNGU, UNATEGEMEA UHUSIANO WAKO NA MWENZI WAKO

Na: Patrick Sanga
Biblia katika kitabu cha Mwanzo 2:18 inasema ‘Bwana Mungu akasema, si vema huyo mtu awe peke yake, nitamfanyia msaidizi wa kufanana naye’. Ni kusudi na mpango wa Mungu watu waoe na kuoana. Hii ni kwa sababu kufanikiwa kwa kusudi la Mungu duniani kunategemea ndoa au wanandoa pia. Naam kwa Mungu ni muhimu sana kujua nani anakuwa mwenzi wako wa maisha tegemeana na kusudi lake la kukuumba.
Tunapoenda kufunga mwaka nimesikia ndani kuweka ujumbe huu kwenye blog hii nikiamini utawafaa wengi. Jambo la msingi ambalo nataka ulipate ni kuhusu uhusiano uliopo kati ya ‘uhuru’ wa kumtumikia Mungu na ndoa yako. Pengine si wengi wanaojua umuhimu wa mahusiano mzuri baina yao kama wanandoa na kumtumikia Mungu. Naam ndiyo maana kuna ujumbe huu kwa ajili yako.
Watumishi wengi katika nyakati za leo hawajawapa heshima na nafasi ambayo wenzi wao wanaistahili. Baadhi ya wanaume wameona kupata mke ni sehemu ya kukamilisha sifa za utumishi wao kama wanandoa bila kujua kwa nini ameunganishwa na huyo mwenzi wake. Wengine wamekuwa wakiwapuuza wake au waume zao na bado madhabahuni wanalihubiri neno. Na kuna baadhi yao hawana upendo kwa wake zao, wake nao  si watiifu kwa waume zao, ni watu wa kugombana, wenye uchungu ndani yao nk, naam bila kutengeneza au kumaliza tofauti zao hizo  utawakuta madhabahuni wakihudumu kwa raha kabisa. Je, jambo hili ni sahihi kweli? Je ni jambo la kumpendeza Bwana?
Fahamu kwamba ‘uhuru wako katika kumtumikia Mungu kwenye nafasi aliyokupa katika mwili wake, ipo kwa mwenzi wako wa maisha’. Ilikuwa Desemba 28, 2010, Bwana Yesu aliponifundisha jambo hili. Naam uhuru wako wa kumtumikia Mungu upo kwa mke/mume wako. Hivyo kama mahusiano yako na mwenzi wako si mazuri huwezi kutumika katika mapenzi yake. Naam uhuru wa wewe kusikia na kupokea kutoka kwa Mungu unategemea sana mahusiano yako na mwenzi wako.
Nilipofuatilia tafsiri ya neno hili uhuru (freedom) niligundua zipo tafsiri nyingi lakini nikachukua hizi tatu kwa kuwa zinaendana na ujumbe huu.  Tafsiri moja wapo ya ‘Oxford dictionary’ inasema uhuru ina maana ya ‘special privilege or right of access’.  Na tafsiri ya neno hilo kutoka katika ‘Encarta dictionary’ ni ‘right to use or occupy a space’ na pia tafsiri nyingine ni ‘ease of movement’.
Naam mahusiano yako na mwenzi wako yanapokwa mazuri jambo hili linakupa haki, kibali, nafasi na mpenyo wa kumtumika Mungu katika kiwango alichokusudia na zaidi katika mapenzi yake. Jambo hili linakupa mpenyo wa kusikia, kuhoji na kusemezana na Mungu juu ya kile ambacho anataka uwafundishe watoto wake ama ukiwa madhabahuni, au kwa njia ya kuandika, kushuhudia nk. Naam kwa hiyo mahusiano mazuri kati yako na mwenzi wako ni ufunguo wa wewe kumtumika Mungu.
Si hivyo tu bali mahusiano yako na mwenza wako yanapokuwa mazuri utapata wepesi wa kutembea na kutumika katika kusudi la Mungu. Naam ndivyo unavyopata haki ya kutumia kila ambacho Mungu ameweka ndani yako kwa utukufu wake, naam ndivyo unavyokuwa na nguvu ya utawala kwenye nafasi na eneo lako la utumishi katika ulimwengu wa roho.
Biblia inasema katika 1Petro 3:7 ‘Kadhalika ninyi waume, kaeni na wake zenu kwa akili; na kumpa mke heshima, kama chombo kisicho na nguvu; na kama warithi pamoja wa neema ya uzima, kusudi kuomba kwenu kusizuiliwe’.
Naamini umeona kile kipengele cha mwisho kinavyosema. Hii ina maana kama mwanaume atashindwa kukaa na mke wake kwa akili na kumpa heshima, maombi yake yatazuiliwa. Sasa fikiri mwanaume huyu ni mtumishi yaani Mchungaji, Mwalimu, Nabii nk nini kitatokea kwa wale anaowachunga au kuwahudumia? Naam mahusiano yako na mwenzi wako ni ya maana sana kama unataka kutumika katika mapenzi ya Mungu. Mahusiano mazuri baina yenu yanaleta mawasiliano mazuri baina yako kama Mtumishi na Mungu wako. Hivyo msingi wa mawasiliano mazuri na Mungu wako, upo kwa mwenzi wako.
Ni vizuri ukafahamu kwamba bila kuwa na mahusinao mazuri na mwenzi wako wa maisha, utumishi wako ni bure. Naam uhuru wako katika kumtumika Mungu unategemea uhusiano wako na mwenzi wako. Si rahisi kwa Mungu kusema na wewe kama mahusiano yako na mwenzi wako si mazuri, matokeo yake utawasikizisha/hubiri/fundisha watu mawazo yako na pengine ya adui, zaidi utahudumu kwa mazoea bila uwepo wa Bwana, au chini ya kiwango cha upako uliokusudiwa, tena ni kwa sababu Mungu anawaonea huruma watu wake.
Jifunze kufanya tathimini ya mahusiano yako na mwenzi wako mara kwa mara, na kuhakikisha unayaboresha, naam jambo hili ni muhimu sana kwenu binafsi na zaidi kwa Mungu ili kupata uhuru wa kusikia kutoka kwake kila wakati kwa ajili yenu na  wale ambao amekupa kuwahudumia.
Nakutakia utumishi mwema katika nafasi yako pamoja na mwenzi wako, mwenzi wako ni wa muhimu sana, mpe nafasi yake, utaona mabadiliko kwenye utumishi wako.

NAMNA MWANAMKE ANAVYOWEZA KUTUMIA NAFASI ZAKE KUBADILISHA MAISHA YA NDOA YAKE



NAMNA MWANAMKE ANAVYOWEZA KUTUMIA NAFASI ZAKE KUBADILISHA MAISHA YA NDOA YAKE

Na: Patrick Sanga
Mithali 14: 1 ‘Kila mwanamke aliye na hekima hujenga nyumba yake; Bali aliye mpumbavu huibomoa kwa mikono yake mwenyewe’.
Mchungaji mmoja rafiki yangu aliniambia asilimia hamsini mpaka sabini ya changamoto au matatizo anayoshughulika nayo mara kwa mara katika kanisa lake ni ya wanandoa. Kwa lugha nyepesi asilimia 50 – 70 ni matatizo yatokanayo au yanayohusiana na ndoa. Binafsi pia kwa upande wangu kupitia nafasi yangu katika mwili wa Kristo, email za wasomaji ninazopata na pia baadhi ya semina za ndoa ambazo nimefanya kuhusu eneo hili nimegundua kwa hakika ndoa nyingi za wana wa Mungu zina shida na wao hawajajua kwamba vita hii inatoka kwa Shetani, maana anajua ndoa zikitengamaa ni faida kwa ufalme wa Mungu na ni uharibifu kwenye ufalme wake wa giza. Naam anapigana usiku na mchana ili kuhakikisha ndoa hazitengamai kwa kuleta fujo za kila aina.
Kila siku katika ndoa kuna changamoto zinazaliwa mpaka imefika mahala baadhi ya wanandoa wanawaza kwa nini walikubali kuoa au kuolewa. Kwa hakika laiti Biblia ingetoa mwanya kwa wanandoa kuachana basi kuna baadhi ya wanandoa wangehakikisha wanaitumia hiyo nafasi vizuri kwa kuwa ndoa zimegeuka ndoano. Matarajio ambayo kila mmoja alikuwa nayo kwenye ndoa anaona hayatimii. Kinachosumbua watu wengi ni kwamba kabla hawajaonana hawakujua nini kinakuja kupitia ndoa, hawakuweza kuona uhalisia wa maisha ya ndoa utakuwaje? Bali kila mmoja alikuwa na mtazamo/fikra na matarajio yake binafsi juu ya ndoa yake.
Naam zipo sababu nyingi sana zinazopelekea matatizo au changamoto kwa wanandoa. Katika somo hili nitaandika zaidi zile zinazotokana na upinzani kutoka kwa Shetani ili kuathiri kusudi la Mungu. Lengo la ujumbe huu ni kukufundisha wewe mama (Mwanandoa) namna ya kuzitumia ‘nafasi’ ambazo Mungu amekupa Kibiblia ili kuiponya ndoa yako au kubadilisha hali ya sasa ya ndoa yako endapo unaona si ile ambayo Mungu amekusudia.
Kwa nini Mwanamke?
Pengine utaniuliza kwa nini mwanamke ndiye awajibike katika kuponya au kubadilisha maisha ya ndoa yake? Binafsi katika kuisoma Biblia nimegundua kwamba kwa kuzingatia nafasi ambazo mwanamke amepewa kibiblia ni ishara ya kwamba kwa habari ya  ndoa, Mwanamke ana nafasi kubwa ya kuijenga au kuibomoa ndoa yake na hivyo nyumba yake kwa ujumla. Mara kwa mara Mungu ananifundisha masuala ya wanawake, suala la wanawake kuwa kwenye ‘nafasi zao’ husisitizwa sana.
Kwa nini nafasi?
Sijui kama unafahamu maana ya nafasi ambayo Mungu anampa mtu katika ulimwengu wa roho. Hizi ni nafasi ambazo Mungu amekupa wewe mawanamke katika ulimwengu wa roho ili uzitumie kufanikisha kusudi lake kupitia ndoa yako. Nafasi (position) ni eneo ambalo mtu anapaswa kuwepo kwa kuhusianisha na vitu au watu wengine, naam ni wadhifa ambao mtu anakuwa nao kwa kuhusianisha na mtu au watu wengine.
Kwa hiyo hizi ni nafasi ambazo Mungu amempa mwanamke zikihusiana na mwanaume katika kilitumika kusudi la Mungu hapa duniani. Mwanamke anapokuwa amesimama katika nafasi zake ndipo anapoweza kuruhusu mawazo ya Mungu kupitia ndoa yake kutimia naam ndivyo anavyoweza kuzuia mawazo ya Iblisi kupitia ndoa yake yasitimie. Naam nafasi ya mwanamke katika ndoa ndiyo inayoamua uzima au mauti ya ndoa yake, nafasi ndiyo inayopelekea kufanikiwa au kufeli kwa ndoa yake, nafasi ya mwanamke katika ndoa ndio inayoamua nini kingie au kitoke kwenye ndoa.
Katika kusoma kwangu Biblia nimegundua kwamba Mungu amempa nafasi zifuatazo mwanamke;
  • Mwanamke kama ‘msaidizi’ wa mumewe
  • Mwanamke kama ‘mlinzi’ wa mwanaume
  • Mwanamke kama ‘mjenzi’ wa nyumba yake
  • Mwanamke kama ‘mshauri’ wa mumewe
  • Mwanamke kama ‘mleta kibali’ kwa mumewe
Naam kutokana na changamoto zinazoendelea katika ndoa mbalimbali nimelazimika kuanza kuandaa mfululizo huu wa namna mwanamke anavyoweza kusimama kwenye nafasi zake na kuiponya ndoa yake. Jukumu langu kubwa itakuwa ni kufafanua kila nafasi ambayo mwanamke amepewa na namna anavyoweza kuitumia hiyo nafasi kubadilisha ndoa yake ambayo anaona inaangamia.
Somo litaendelea, maombi yako ni muhimu sana.

JE, MAAMUZI YA NANI ATAKUWA MWENZI WAKO WA MAISHA NI YA MUNGU AU YA KWAKO?



JE, MAAMUZI YA NANI ATAKUWA MWENZI WAKO WA MAISHA NI YA MUNGU AU YA KWAKO?

 Na: Patrick Samson Sanga.
 Mithali 19:14 “Nyumba na mali ni urithi apatao mtu kwa babaye; bali mke mwenye busara mtu hupewa na Bwana”.
Ni matumaini yangu kwamba u-mzima kijana mwenzangu na una maendeleo mazuri kiroho na kimwili. Katika waraka huu mfupi kwa vijana nataka kujibu swali hili ambalo vijana wengi wamekuwa wakijiuliza. Wengine kutokana na kutojua ukweli wake wamejikuta wakifanya maamuzi ambayo hadi leo wanayajutia .
Kibiblia, tunajua kabisa ni mpango wa Mungu tuweze kuoa au kuolewa. Sasa swali linakuja, je ni lazima Mungu anionyeshe, anipe mke au mume wa maisha yangu? Kwani mimi kijana sina uwezo wa kuangalia mtu kisha nikaomba Mungu na mwisho nikajichagulia mwenyewe? Au kifupi maamuzi ya nani atakua mume/mke wangu ni ya nani?
Hili ni swali ambalo vijana wengi limekuwa likiwachanganya. Wengine wanaamini maamuzi hayo ni ya Mungu kunipa mke/mume na wengine wanaamini Mungu hahusiki, bali wao ndio wenye nafasi na wanaohusika. Sasa hayo ni mawazo yao wala mimi sitaki kuyapinga lakini ngoja nikuonyeshe Biblia inasema nini halafu utajua ukweli ni upi:-
Kwenye kitabu cha Mithali 19:14 , Mungu anasema suala la nyumba, mashamba, maduka na vyote vifafanavyo na hivi nimewapa uwezo na ruhusa wazazi wako baba & mama) wa mwili wakupe lakini suala la mke au mume mwenye busara mimi pekee ndiye ninaye wajibika kukupa .Sikiliza kama unataka mke/mume kwa ajili ya kulitumikia kusudi la Mungu alilokuumbia basi huna budi ni lazima upige goti kuomba na kisha ungoje Mungu akuonyeshe/ akupe mke/mume wa kusudi lake.
Vijana wengi wanafikiri eti kwa sababu wameokoka, na wamejzwa roho mtakatifu basi wanao – uwezo wa kujichagulia mke/mume wa kuishi nao. Sikiliza kama una amini umeumbwa kwa kusudi la Mungu na unataka kutembea katika njia yake basi mruhusu Mungu akupe mke/mume mwenye busara ya kukaa na wewe.
Mke au mume ana sehemu kubwa katika maisha yako. Anaweza akabadilisha maisha yako, ya kiroho, kiuchumi, kimwili, kihuduma na kima husiano na watu wengine.Hivyo kibiblia maamuzi ya nani atakuwa mkeo au mumeo ni ya Mungu na si ya kwako. Hii ina maana ukimuomba Mungu hakika atakuletea mtu halisi wa kukaa na wewe. Lakini maamuzi ya kumkubali au kumkataa ni ya kwako na si ya Mungu. Ukikubali shauri la Bwana litatumikiwa, ukimkataa, umejikaribishia laana.
Zifuatazo ni sababu za msingi zinazomfanya Mungu akuchagulie/akupe mke/mume na sio kukuruhusu wewe/wazazi/ukoo wako/mchungaji wako kukuchagulia mke.
(a)Kusudi la uumbaji (kuwaunganisha) .
Sikiliza hakuna mtu aliyeumbwa kwa bahati mbaya, Mungu ndiyo aliyekuchagua na siyo wewe uliyemchagua na akakuweka duniani ili umtumikie sasa yeye ndiye anayejua nikimuunganisha huyu kaka na yule dada watalitumikia kusudi langu.  Warumi 8:28-29.  Mungu anapofanya maamuzi anafanya kwa kuangalia kusudi lake na muda na wahusika wa hilo kusudi. Yeye ni Mungu na anafanya kwa utikufu jifunze kuruhusu mapenzi ya Mungu yatimie na si ya kwako.
(b) Mungu ndiye ana-fahamu nani mwenye busara ya kukaa na wewe.
Mithali 19:14b Busara ni uwezo uliomo ndani ya mtu (mke/mume) unaomsaidia kujizuia kufanya jambo ambalo liko nje ya mpango/mapenzi ya Mungu kwa kufanya lile lilio katika mapenzi ya Mungu.Hivyo Mungu pekee ndiye anaye mjua mke/mume mwenye busara ya kukaa na wewe, kamwe wewe hutaweza mjua bila uongozi wa Mungu.
(c) Sababu za ki-Agano.
Zaburi: 32:8 Siku uliyofanya maamuzi ya kuokoka maana yake uliyakabidhi maisha yako kwa Yesu, ukamwambia nafungua moyo wangu uingie uyatawale na kuyaongoza maisha yangu sasa hilo ni Agano lako kwa Mungu. Kwa sababu hiyo Yesu anawajibika kwako kukufundisha na kukuonyesha njia utakayoiendea, hii ikiwa ni pamoja na kukupa mke/mume wa kukufaa.
(d)Mawazo yake, si mawazo yako.
Isaya 55:8 Sikiliza Mungu anayo mawazo (mipango) na njia (mikakati) ya kukufanikisha kimaisha. Sasa katika kutekeleza mipango yake kwako na kupitia wewe lazima atumie mikakati yake ili kutekeleza mawazo yake. Sasa moja ya mikakati yake ni kukupa mke au mume wa kusudi lake .
Sasa, sikatai huenda kwa jinsi ya mwili ni kweli huyo mtu anayekupa Mungu ana upungufu fulani. Huenda umbile lake, sura yake, kabila lake, rangi yake, dhehebu lake, haliko
 kama ulivyo kuwa unavyotaka wewe. Mungu anakupa mke au mume kutokana na sababu hizo ambazo nimekuekezea hapo juu na ninakuhakikishia ukimkubali atakupa neema ya kukaa naye huyo mtu na kukufanya uridhike naye na kumpenda huyo mwenzako .
Nakutakia uongozi wa Mungu katika eneo la maamuzi ya nani atakua mumeo au mkeo .

MAKOSA WANAYOFANYA VIJANA KATIKA KUTAFUTA MWENZI WA MAISHA.



MAKOSA WANAYOFANYA VIJANA KATIKA KUTAFUTA MWENZI WA MAISHA.

KWA NINI VIJANA WENGI WANAKOSEA KATIKA KUTAFUTA MWENZI WA MAISHA?
Maamuzi ya kuoa au kuolewa, si maamuzi madogo, ni moja ya maamuzi makubwa ambayo vijana wengi wa kike na wa kiume wana kutana nayo kila siku. Sasa katika kufanya maamuzi haya ukweli ni kwamba sehemu kubwa ya vijana mpaka wafike mahali pa kumpata kijana au binti wa kusema huyu ndiye haswa wa kutoka kwa Bwana, basi ujue tayari wengi wanakuwa walishakosea mara nyingi mpaka kufikia hapo. Wapo ambao wakikosea husema, yule wa kwanza hakuwa chaguo la Bwana, au haukua ufunuo wa Mungu mwenyewe bali malaika, au utasikia mwingine akisema Bwana amemchukia Esau akampenda Yakobo au amehamishia upako wa Sauli kwa Daudi kwa maana ya kwamba upako umehama kutoka binti wa kwanza hadi kwa mwingine. Mimi sina uhakika sana na hizi kauli.
Je hivi kweli hayo ndiyo yalivyo au ni ujanja ujanja tu wa vijana tena hasa wa kiume ndio wenye kauli kama hizi. Lengo la waraka huu mfupi kwako kijana mwenzangu ni kutaka kukueleza sababu kadhaa ambazo kupelekea vijana wengi kufanya makosa katika kutafuta mwenzi wa maisha.
*Wengi wanakuwa tayari wameshafanya maamuzi ya nani ataishi naye.
Vijana wengi huwa wanaomba Mungu awape mtu sahihi wa kuishi naye na wakati huohuo tayari kwenye nafsi yake anakuwa na mtu wake kwamba lazima huyu tu ndiye nitaishi naye. Na kwa sababu hiyo ina kuwa ni vigumu kwao kumpata mtu wa mapenzi ya Mungu na pia ina muwia kazi Mungu kukuonyesha mke au mme wa kusudi lake kwani tayari umeshafanya maamzi ndani yako, je Mungu afanye nini kama sio kunyamaza.
*Sababu za kipepo
Hapa nitaelezea mambo mawili kwa wakati mmoja, la kwanza ni hili kuna vijana huenda wao wenyewe au ndugu zake, wazazi wake walishawahi kumtoa huyo mototo kama dhabihu kwa mapepo kwa sababu ya mila zao au pia alipatikana kwa njia za kipepo. Siri moja ni hii kuna baadhi ya mapepo huwa hayapendi kushare sex na mtu mwingine, hivyo ni lazima yalete kila namna ya upinzani ili mtu asiolewe na wala kuoa. Na mwingine hata kama hakutolewa kama dhabihu lakini huenda pepo wameshawahi kufanya mapenzi na huyo mtu na kama yatampenda basi ujue hayatakubali aolewe au kuoa, hivyo yatamletea kila namna ya upinzani katika kuolewa au kuoa kwake. Mengine hufika mahali hata pa kumwachia kijana wa watu harufu mbaya ili mwingine asimpende.
*Maneno ya kujitamkia
Kuna baadhi na hasa hapa ni akina dada kwa sababu mbalimbali kama vile kubakwa, kujeruhiwa katika nafsi kwa sababu ya kuachwa na mchumba wake hufikia mahali wakasema mimi sitaki tena kuolewa. Sasa inpofika muda umepita na wanataka tena kuolewa wananaza kuomba Mungu awape mume, wakati huo wamesahau kwamba walishatamka kwamba hawataki tena kuolewa. Nisikilize ukisema hutaki kuolewa au kuoa tena, maana yake unaifunga nafsi yako hapo kwamba hutaoa kuolewa, na Biblia inasema mtu atashiba matunda ya kinywa chake. Na wakati huo shetani ni mwepesi kufuatilia maneno ambayo ni ya athari kwako. Sasa bila kufuta kwa Damu ya Yesu ndugu utakesha hapo.
*Dhambi.
Sikiliza Biblia inasema afichaye dhambi zake hatafanikiwa, (Mithali 28:13a). Kuna baadhi ya vijana huwa wanakuwa awali kuna baadhi ya dhambi wamezifanya na hawajazitubia, na bado wana taka mtu awaoe au wa kumwoa. Biblia iko very clear kama kuna dhambi umeficha hutafanikiwa, sasa inategemeana, lakini pia inahusiana sana na kutofanikiwa kwako pia kumpata hata mwenzi tu. Nikupe mfano mara nyingi watu wanatoa mimba, au watoto wanaozaa, nao pia kupata mume au mke huwa inakuwa kazi kweli kweli.
*Kutokuenenda kwa Roho.
Paulo anasema, “Basi nasema enendeni kwa roho wala hamtatimiza kamwe tama za mwili” (Wagalatia 5: 16). Kuenenda wa Roho maana yake ni kuongozwa na Roho Mtakatifu, hii ni pamoja na zoezi zima la kutafuta mke au mme. Sasa kwa sababu wewe unaenda kwa mwili, mara eti nataka mtoto portable, mguu wa chupa, mweupeee, nk. Hivyo vitu unavyotaka wewe kuna wengine pia wanataka hivyohivyo na matokeo yake mnaanza kugombaniana msichana au mvulana kwa sababu tamaa za miili yetu zinawaongoza huko.
*Kuwa na vigezo binafsi.
 Vijana wengi sana katika suala zima la kupata mke ua mme, ukweli wengi wao wana vigezo vingi sana ambavyo kila mmoja angependa huyo mchumba wake awe navyo. Utasikia lazima awe wa kabila ya kwangu, awe portable, mweupee, mrefu ndio mzuri, ajue kutabasamu na kisha awe ana ulamba. Sawa mi sikatai hivyo vigezo, lakini nikuulize swali Je! Unayajua mawazo ya Mungu kuhusu wewe kwa habari ya mkeo au mmeo? Je kibiblia hivyo vigezo vyako vinakubalika/ na je mke/mme mtu huchagua mwenyewe au hupewa na Bwana?
 Najua utaniambia mimi nitaomba Mungu anipe mke/mme mwenye sifa hizo. Ok. Ukiniambia hivyo na mimi nitakuambia kumuomba Mungu kwa muundo huo ni nzuri kabisa, wala sio dhambi lakini kumbuka maandalio ya moyo ni ya mwanadamu lakini jawabu la ulimi hutoka kwa Bwana. Na hapo ndipo patamu, wengi huwa wanaomba kwa vigezo vyao, na mara nyingi Mungu anapojibu inakuwa tofauti na vigezo vyao, na hapo wengine wanakataa hata chaguo la Bwana wanabakia kuteseka. Jua kwamba wewe unapoweka vigezo vya mwenzi wako na Mungu naye ana vigezo vya aina ya mwenzi anayekufaa.
* Kufanya maamuzi kabla ya wakati.
Biblia inasema katika Mhubiri 3:1 “kwa kila jambo kuna majira yake, na wakati wa kila kusudi chini ya mbingu”.Hili ni jambo la kawaida, hata wakati wa uchaguzi kura mtu harusiwi kupiga kama hajafikisha miaka kumi na nane kwa nchi nyingi. Vivyo hivyo hata suala la kutafuta mke au mume lina wakati wake maalumu. Ukitaka kulifanya nje ya kipindi ambacho Mungu amekipanga kwa ajili yako utateseka hadi uchoke. Kumbuka kila mtu ana muda wake, hivyo basi hakuna muda maalumu wa kila mtu kuanza kutafuta mke au mme, bali kila mtu ana muda wake na mara tu unapowadia Mungu humjulisha mtu wake.
Nisikilize ukiulekeza moyo wako upate kujua haya nisemayo na ukajizuia kufanya makosa kama haya, basi nataka nikuhakikishe suala la kupata mke au mme wa kutoka kwa Bwana litakuwa ni jepesi sana,ni sawa sawa na kuombea chakula na ukishafumbua macho ukaanza kula moja kwa moja ukiwa na uhakika kimeponywa na kubarikiwa.
Ndimi katika huduma hii,
Sanga P.S.


ANGALIA MAAMUZI UNAYOFANYA KATIKA KUTAFUTA MWENZI WA MAISHA YASIHARIBU KUSUDI LA MUNGU KWAKO.

 
Na : Sanga P.S

Isaya 55: 8 “Maana mawazo yangu si mawazo yenu, wala njia zenu si njia zangu; asema Bwana”.

Najua yamkini umeusoma au kusikia na hata kuufundisha sana huu mstari. Lakini leo katika kona  hii ya ndoa nataka nikuonyeshe tafsiri ya huu mstari kwa kadri ya neema ambayo Bwana amenijalia kwenye hili eneo. 

Ukisoma vizuri huu mstari utagundua kwamba kulikuwa na ushindani/ kutofautiana kimawazo kati ya Mungu na hawa watu anaowasema hapa. 

Yeremia 29:11 inasema “maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi asema Bwana….” Sasa ukiunganisha maneno ya Yeremia 29:11 na yale ya Isaya 55: 8 utagundua kuna mawazo na njia za kutekeleza hayo mawazo  ambazo Mungu alikuwa nazo juu ya maisha ya hawa watu.

Sasa tatizo na wao kuna mawazo na njia walikuwa nazo juu ya maisha yao ambazo hazikuwa sawasawa na zile za Mungu. Na ndiyo maana akasema mawazo yangu si mawazo yenu, wala njia zenu si njia zangu. Kwa lugha rahisi Mungu alikuwa akisema geukeni/acheni hayo mawazo (mipango) na njia zenu tekelezeni mawazo yangu na njia zangu ndipo mtafanikiwa. Mungu alisema hayo maneno bada ya kuona matokeo ya mawazo na njia zao ni mabaya, kwa kuwa yalikuwa nje ya kusudi lake juu yao.

Ukitaka kuthibitisha kauli hii soma ule mstari wa 7 katika Isaya 55 Biblia inasema “Mtu mbaya na aache njia yake, na mtu asiye haki aache mawazo yake; na amrudie Bwana naye atamrehemu, na arejee kwa Mungu wetu naye atamsamehe kabisa”.
Anaposema mtu mbaya/asiye haki anamaanisha mtu ambaye anataka kutekeleza mawazo na njia ambazo zipo kinyume na mawazo na njia za Mungu juu ya maamuzi/suala/jambo lolote linalomkabili huyo mtu.

Maana yake nini mambo haya?

Katika maamuzi ya kupata/kutafuta mwenzi wa maisha najua kabisa  kuna mambo/vitu ambavyo ungependa huyo mwenzi wako awe navyo. Kuna namna fulani ungetamani awe kiumbile, kiumri, kikabila, kielimu, kiutajiri, nk, kwa kifupi tuseme haya ni mawazo yako juu ya mwenzi wako wa maisha . Niseme kwamba ni kweli haya ni mawazo yako lakini usifikiri Mungu naye hana mawazo ya nani anastahili/anafaa kuwa mwenzi wako wa maisha. Hakika Mungu anayo  mawazo tena mazuri kabisa juu ya nani anafaa kuwa mwenzi wako.

Hii ni  kwa sababu yeye ndiye aliyekuumba na ndani yako ameweka kusudi lake ambalo anataka litekelezwe kwa njia au mikakati yake. Moja ya mikakati hiyo ni kuhakikisha unoa au kuolewa na mtu aliyemkusudia yeye.
Jifunze kuruhusu mawazo ya Mungu na njia za Mungu zitekelezwe katika maisha yako,  ili kusudi lake liweze kufikiwa.

 .
Kumbuka Mithali 16:1 inasema, maandalio ya moyo ni mwanadamu, bali jawabu la ulimi hutoka kwa Bwana. Unaweza kupanga au kuamua aina ya  mwenzi unayemta na ukaweka sifa/vigezo kadha wa kadha lakini  Kibiblia/Ki- Mungu SI LAZIMA iwe kama ulivyopanga kwa sababu mwenye kutoa jawabu la ulimi juu ya maandalio ya moyo wako ni Mungu.

Nimalizie kwa kusema kazi ya Roho mtakatifu ni kukushauri na kukuongoza  na si (kukulazimisha) katika yaliyo mapenzi ya Bwana. Hivyo hata katika suala la mwenzi wako yeye atafanya wajibu wake ikiwa utamruhusu. Maamuzi yanabakia kwako kutekeleza mawazo na njia zake kwako, ukikakataa uwe na hakika umekaribisha  mabaya na kutotendewa haki katika ndoa yako sawasawa na Isaya 55:7 na mwisho wenu ni majuto.

Mpendwa wangu angalia sana maamuzi unayotaka kufanya, hakikisha yamepata kibali cha Bwana ukikumbuka haya ni maamuzi makubwa na yanagharimu sana.

Nakutakia safari njema katika hili, tukumukane katika maombi.