IJUE NA KUITUMIA NAFASI YAKO KAMA MLINZI KWENYE ULIMWENGU WA ROHO (Part 3)
(Umuhimu wa taarifa na mahusiano mazuri baina ya mlinzi na watu wa eneo lake)
Na: Patrick Sanga
Ili kusoma sehemu ya pili bonyeza link hii http://sanga.wordpress.com/2011/12/07/ijue-na-kuitumia-nafasi-yako-kama-mlinzi-kwenye-ulimwengu-wa-roho-part-2/
Katika
sehemu ya pili naliahidi kwamba ningeanza kuelezea kuhusu nafasi
mbalimbali za ulinzi, lakini ndani yangu nimesikia kuandika mambo kadhaa
yafuatayo tena kabla sijaanza kuandika kwa habari ya nafasi husika. Ni
imani yangu kwamba sehemu ya nne itaanza kwa kuelezea nafasi husika,
fuatana nami tuendeleae.
Jambo ambalo nimesukumwa niandike kwa habari ya eneo hili la tatu ni umuhimu wa taarifa na mahusiano mazuri baina ya mlinzi na watu wa eneo lake.
Jambo la kwaza – Umuhimu wa taarifa ya mlinzi kwa watu wa eneo lake
Hebu tuangalie jambo hili kupitia
kitabu cha Mathayo 25:1-13. Hii ni habari ya wanawali kumi waliokuwa
wakimsubiri Bwana Harusi. Biblia inatuambia watano kati yao walikuwa na
busara na watano walikuwa wapumbavu. Busara ya wale watano wa kwanza ni
kuwa na taa zenye mafuta ya akiba huku wakimsubiri Bwana, na upumbavu wa
wale watano wengine ni kuwa na taa zisizo na mafuta ya akiba huku
wakimngoja Bwana harusi pia.
Kwa sababu ya Bwana harusi kuchelewa wanawali hawa wote waliamua kulala. Ule mstari wa sita na saba inasema ‘Lakini
usiku wa manane, pakawa na kelele, Haya, Bwana arusi; tokeni mwende
kumlaki. Mara wakaondoka wanawali wale wote, wakazitengeneza taa zao’.
Katika sehemu ya pili ya somo hili
niliandika kwamba jifunze kuitazama taarifa ya mlinzi kama fursa ya
matengenezo. Biblia iko wazi kwamba wanawali hawa waliamua kulala baada
ya kuona Bwana harusi wao amechelewa. Kumbuka kwamba lengo la wote hawa
ilikuwa ni kumlaki Bwana Harusi. Sasa kilichowaamsha toka usingizini ni ‘kelele za taarifa’ ambazo ninaamini zilikuwa za walinzi ambao jukumu lao ilikuwa ni kutoa taarifa juu ya uwepo au ujio wa Bwana harusi husika.
Kutokana na mfano huu tunajifunza
kwamba mosi taarifa ya mlinzi/walinzi iliwasaidia wanawali kuamka kutoka
usingizini maana walikuwa wamelala. Licha ya taarifa kuwasiaida kuamka
usingizini, taarifa ya mlinzi ilitoa fursa ya wanawali kujiandaa.
Tumeona katika mstari wa saba kwamba punde baada ya taarifa wale
wanawali wakaamka na kuziandaa/zitengeneza taa zao. Naam taarifa ya
walinzi ilitoa fursa ya matengenezo. Hivyo hata sasa Mungu anapoleta
taarifa kwako, ujue analeta taarifa ya matengenezo, naam mbele kuna
jambo linakuja, hivyo analeta taarifa mapema kupitia walinzi wako au wa
eneo lako ili uitumie kutenda yapasayo.
Jambo la pili – Umuhimu wa kuwa na mahusiano mazuri kati ya Mlinzi na watu wa eneo lake.
Kupitia mfano huu wa wanawali kumi
tunagundua pia kwamba, taarifa ya mlinzi ilitoa fursa ya mawasiliano
baina yao. Kabla ya taarifa hatuoni wanawali hawa wakiwasiliana kwa
jambo lolote. Si hivyo bali pia tunagundua kwamba baada ya taarifa ya
mlinzi ndipo fahamu za wale wanawali wapumbavu zikafunguka na wakajua
mafuta yao hayatoshelezi. Kwa mujibu wa Biblia harusini aliruhusiwa
kuingia mtu (mwanamwali) mwenye taa inayowaka yaani taa yenye mafuta.
Je, ni kwa nini wale wanawali
wapumbavu kabla hawajaenda kulala hawakufikiri kwamba mafuta haya
yakiisha na hatuna ya akiba hatuwezi kuingia harusini? Huenda hawakujua
kwamba mwanamwali mwenye taa inayowaka ndiye atakayeruhusiwa kuingia
harusini. Jambo ninalotaka ulione ni kwamba pamoja na kutokujua kwao,
walinzi wa mji walijua nini kinatakiwa kwa mtu kuingia harusini. Laiti wanawali wangekuwa na mahusiano mazuri na walinzi wa mji wangepewa siri kuhusu ujio wa Bwana harusi wao.
Lakini kwa sababu hawakuwa na mahusiano mazuri na walinzi, walishindwa
kuwauliza wale walinzi mahitaji ya msingi atakapokuaja Bwana harusi.
Naam wakajikuta wameachwa na Bwana wao walipoenda kutafuta mafuta.
Ukweli huu kuhusu mahusiano unathibitishwa katika kitabu cha Wimbo Ulio Bora 3:3 unaosema ‘Walinzi wazungukao mjini waliniona; Je! Mmemwona mpendwa wa nafsi yangu’.
Habari hii inatueleza habari za kijana aliyekuwa anamtafuta mwenza
(mpenzi) wake kwa muda mrefu bila mafanikio. Katika kuendelea kumtafuta
ndipo akakutana na walinzi wa mji, akawauliza mmemwona
mpendwa wa nafsi yangu? Ni imani yangu walinzi wale walimjibu,
kwa sababu mstari wa nne unatumabia ‘kitambo kidogo tu nikishakuwaondokea, nikamwona mpendwa wa nafsi yangu, Nikamshika nisimwache tena…’
Hivyo ufumbuzi wa tatizo (hitaji) la huyu kijana ulipatikana kwa
walinzi wa mji. Kwa hakika mahusiano mazuri ya Walinzi na yule kijana
yalipelekea hitaji la kijana kufanikiwa au kufikiwa.
Kutokana na habari hii ni dhahiri kwamba walinzi
wamewekwa kwenye nafasi zao ili kuleta ufumbuzi juu ya changamoto
zinazomkabili mwanadamu kwa kumjulisha mawazo ya Mungu juu yake, ili pia
kumsaidia mwanandamu aishi kwa kulitumikia shauri la Mungu katika siku
zake. Biblia katika kitabu cha Isaya 62:6-7 inasema ‘Nimeweka
walinzi juu ya kuta zako, Eee Yerusalemu; hawatanyamaza mchana wala
usiku; ninyi wenye kumkumbusha BWANA, msiwe na kimya; wala msimwache
akae kimya, mpaka atakapoufanya imara Yerusalemu, na kuufanya kuwa sifa
duniani’.
Mungu anataka yawepo mawasiliano na
mahusiano mazuri kati ya Mlinzi (Walinzi) na wanaolindwa. Katika andiko
hilo hapo juu, licha ya Mungu kuweka walinzi juu ya kuta za Yerusalemu
ilibidi awape taarifa na wakazi wa mji huo, ili wasije, walinzi hao
wakatoa taarifa ya kile Mungu amesema na wakazi wa Yesrusalemu
wakapuuza, mwisho wao wakaangamia.
Ukisoma pia Biblia katika kitabu cha Mathayo 24:43 inasema ‘Lakini
fahamuni neno hili; kama mwenye nyumba angalijua ile zamu mwivi
atakayokuja, anagalikesha, wala asingeliacha nyumba yake kuvunjwa’.
Naam kiroho milinzi au walinzi ndio waliopewa uwezo wa kuona nini
kinakuja juu yako, ndoa yako, kazi yako, huduma yako, taifa lako nk. Kwa
sababu hii ni muhimu sana kuwa na mahusiano mazuri na mlinzi au walinzi
ambao Bwana Mungu amekuweka chini ya Mlango au Himaya yao. Naam
kufanikiwa kwa kazi ya mlinzi katika nafasi yake kunategemea mahusiano
na ushirikiano anaopata kutoka kwa watu wa eneo lake.
Mungu akubariki kwa kufuatilia mfululizo huu, usiache kuombea muendelezo wa somo hili. Tutaendelea na sehemu ya nne…
No comments:
Post a Comment