Saturday, April 21, 2012

UNAJIFUNZA NINI KUPITIA HUDUMA YA ANANIA NA BARNABA KWA PAULO?




UNAJIFUNZA NINI KUPITIA HUDUMA YA ANANIA NA BARNABA KWA PAULO?

 
Na; Patrick Samson Sanga.
Utangulizi;

Nakusalimu katika jina la Bwana, mpenzi msomaji.

Katika nyanja hii, leo nimeona ni vema tushirikishane kile ambacho Mungu alikifanya  kwa Paulo kupitia huduma ya Anania na Barnaba. Si watu wengi sana wanofahamu nafasi ya Barnaba na Anania kwa Paulo, kwanza mtu mwingine ukimuuliza unawafahamu kina Anania wangapi kwenye kitabu cha Matendo ya mitume wangekutajia Anania, mume wa Safira tu yule aliyeuawa kwa kuiba sadaka ya kiwanja na mkewe.

Nafasi ya Anania na Barnaba kwa Paulo.

Matendo ya Mitume 9: 10 -19 “kulikuwa na Mwanafunzi huko Dameski, jina lake aliitwa Anania……..
Matendo ya Mitume 9:27 inasema “ na Barnaba akamchukua—-‘

Watu wengi sana wanamfahamu vizuri Paulo na kumsifu kwa kazi nzuri aliyoifanya, hata mimi nuaungana na watu wenye mtazamo huo. Lakini si watu wengi pia wanaojua kwamba kazi aliyoifanya Paulo ni matunda ya uaminifu na utiifu wa Anania na Barnaba kwa Mungu wao. Watu wengi wanafikiri Paulo baada ya kuokoka tu, hapo hapo alianza huduma, si kweli wanatheolojia wansema inawezekana Paulo alikaa miaka 14 kwanza ndipo akaanza huduma. Na ukisoma vizuri kitabu cha wagalatia utagundua Paulo alikaa miaka 17 tangu kuokoka kwake na ndipo huduma yake ikapata kibali machoni pa mitume na watu wote.

Sasa katika kipindi hiki cha mpito licha ya kuendelea na huduma, Paulo alikuwa akifunzwa au akielekezwa kitu cha kufanya kupitia watu mbalimbali na hasa Anania na Barnaba. Anania ndio mwanafunzi wa kwanza aliyejenga msingi wa huduma ya Paulo, hii ina maana Anania angekosea huenda huduma ya Paulo ingesumbua pia.

Vivyo hivyo na Paulo alipokwenda Yerusalemu wanafunzi wote walimtenga. Barnaba ndiye aliyemchukua akamtia moyo na kumfariji na kisha akaitambulisha huduma yake kwa mitume na wanafunzi wengine na ndipo Paulo akapata kibali na uhuru wa kufanya huduma hiyo. Unaweza ukaona kama ni kitu kidogo lakini katika ulimwengu wa roho hawa watu waliweka alama kubwa sana na ndio maana hadi leo mimi na wewe tunabarikiwa na nyaraka za Paulo.

Jifunze yafuatayo kupitia ndugu hawa.

Moja, usiidharau nafasi yako mbele za Mungu, kumtumikia Mungu si mpaka usimame madhabahuni ufundishe maelfu ya watu. Wapo waliopewa kusimama madhabahuni lakini pia wapo waliopewa kutengeneza wale watakaosimama madhahuni. Using’ang’anie wajibu usiokuwa wa kwako. Kila mmoja katika mwili wa Kristo ana wajibu wake.

Paulo amejulikana sana lakini mbele za Mungu Anania na Barnaba wanaheshima zao kubwa zaidi kwa kukubali maagizo ya Mungu juu ya Paulo. Haijalishi watu wanaidharau kiasi gani huduma yako, uwe na uhakika Mungu anaithamini sana kazi yako. Huenda wanadamu wasikutukuze au kuona umuhimu, mchango wako katika ufalme wa Mungu bali uwe na uhakika pia Mungu ameiona na kuiheshimu sana kazi yako. Kwa Mungu Anania na Barnaba wana nafasi ya kwanza kuliko Paulo kwa sasbabu wao walikuwa walimu wa Paulo kiroho. Na neno linasema  mwanafunzi hampiti mwalimu wake.

Tekeleza wajibu wako na Bwana Mungu atakubariki katika hilo. Usitafute kuonenkana na watu, tambua kwamba Mungu yu pamoja na wewe. Siku zote zote lenga kutengeneza watu watakaotengeneza na kubadilisha maelefu ya watu. Usibakie kung’anga’nia madhabahu isiyo ya kwako kwa kugombana na wachungaji. Kama Mungu amekuletea hata mtu mmoja kama Anania, tekeleza wajibu wako vema kwa kumfunza huyo. Nani ajuaye huenda atakuwa mfano wa Paulo kwa kizazi cha leo. Sasa ni vema ukae kwenye nafasi yako na ndipo ufanisi wako utakuwa mzuri zaidi. Kadri unavyokuwa mwaminifu kwa huyo mmoja ndivyo Mungu atavyowapitisha na wengine wengi kwako upate kuwajenga na kuwafundisha njia ya Kristo ili waje kuwa watumishi wazuri wa kesho.

No comments:

Post a Comment