Friday, April 20, 2012

JIFUNZE KUFIKIRI KABLA HUJACHUKUA UAMUZI WA KUOA AU KUOLEWA


JIFUNZE KUFIKIRI KABLA HUJACHUKUA UAMUZI WA KUOA AU KUOLEWA

Na: Patrick Samson Sanga
Nawasalimu kwa jina la Yesu . Leo katika nyanja hii ya vijana, nimeona ni vema tukashirikishana kuhusu suala la ‘kufikiri kabla ya kuoa au kuolewa’.
Siku moja katika kusoma Biblia nilikutana na mstari ufuatao, nakusahuri uusome kwa umakini. Biblia katika 1Wakorinto 7:8-9 inasema “Lakini nawaambia wale, wasiooa bado na wajane, Ni heri wakae kama mimi nilivyo, lakini ikiwa hawawezi kujizuia, na waoe, maana ni afadhali kuoa kuliko kuwaka tamaa”.
Baada ya kuusoma mstari huu niliingia katika tafakuri nzito sana ambayo mwishowe ilinipeleka kuandaa somo hili, kwamba ni vema ukafikiri vizuri kabla ya kuchuka uamuzi wa kuoa au kuolewa.
Unajua malezi, dini, madhehebu yetu, wazazi, mila na desturi vinachangia kwa kiwango kikubwa sana kuhusu utaratibu wa kuanzia mtu kupata mke au mume mpaka watakapofunga ndoa. Kila kundi lina mfumo na utaratibu wake ambao lingependa vijana waufuate ili kuhakikisha wanaoa na kuolewa kwa kile ambacho kila kundi linaona na kuamini kwamba huo ndio uataratibu mzuri kufuatwa. 
Namshukuru Mungu kwa kuwa nami nimeoa, ingawa vitu vingi sana Bwana alikuwa ananifundisha vinavyohusu ndoa hata kabla sijaoa. Nakubaliana na dhana kwamba ili uweze kuwa Mwalimu mzuri kwenye nyanja fulani basi ni lazima au ni vema wewe mwenyewe ukawa umepitia kwanza kwenye nyanja hiyo. Lengo ikiwa sio tu ufundishe ‘theory’ bali pia utufundishe na uzoefu wako binafsi kwenye eneo hilo. Licha ya kukubaliana na dhana hii, kwangu binafsi haikuwa hivyo, maana kuna mambo mengi ambayo, Bwana Yesu, alikuwa ananifundisha yanayohusu ndoa hata kabla sijaoa.
Kwa kifupi ndoa ni shule au darasa ambalo wanandoa wanatakiwa kukaa chini na kujifunza kila siku namna ya kuishi humo ndani ili kuweza kuishi maisha ambayo Mungu amewakusudia.
Kutokana na mifumo ya baadhi ya makanisa yetu, si vijana wengi ambao wanafundishwa kwa undani kuhusu maamuzi haya makubwa. Wengi wao wameingia kimwili na kujikuta wakijutia na kulaumu kwa nini nilimuoa au kuolewa na huyu kijana. Nasema haya kwa kuwa nimekutana na wanandoa wengi wa aina hii, na nataka nikuambie kama Biblia ingetoa mwanya wa wanandoa kuachana na kuoa au kuolewa na mtu mwingine, wapendwa wengi sana walioko kwenye ndoa wangefanya hivyo na wengine wasingekubali kuolewa au kuoa tena.
Unajua kwa nini?
Ni kwa sababu si vijana wengi wenye ufahamu wa kutosha juu ya aina ya maamuzi wanayotaka kuyachukua. Kwa hiyo katika somo hili nimeona vema niandike mambo manne ya msingi ambayo naamini yataongeza na kupanua ufahamu wako ili kukusaidia kufikiri kwanza kabla ya kufanya maamuzi haya makubwa;
  • Si kila ndoa inayofungwa imeunganishwa na Mungu, kwa kuwa ndoa ni kiungo cha muhimu kwa Mungu na Shetani pia.
Kuanzia mwaka 2005, Mungu alinipa kibali cha kuanza kufundisha na pia kushauri  juu ya mambo kadhaa kuhusu wanandoa. Tangu wakati huo hadi sasa nimekutana na baadhi ya wanandoa ambao wanajuta kwa nini walikubali kuoa au kuolewa. Wanaishi kwenye ndoa kwa sababu tu ya watoto na pia kwa hofu kwamba endapo kama wataachana jamii na watu wanaowazunguka hawatawaelewa.
Ni vizuri ukafahamu kwamba si kila ndoa inayofungwa ni ya mapenzi ya Mungu, hata kama imefungwa kanisani. Biblia inaposema kilichounganishwa na Mungu, mwanadamu asikitenganishe, katika nafasi ya kwanza maana yake iwe ndoa ambayo Mungu ndiyo aliyehusika katika kuanzisha mahusiano na kuwaongoza hao watu kuishi pamoja. Wakati Mungu anatafuta kuhakikisha watu wake wanaoana katika mapenzi yake na Shetani naye anapambana kuhakikisha watu wanaoana katika hila (mapenzi) zake.
Shetani amefanikiwa kwa kiwango kikubwa sana kuvuruga wanandoa wengi na kuwafanya waishi maisha tofauti na yale ambayo Mungu aliwakusudia. Ni kwa sababu hii ndio maana Paulo aliwaambia Wakorinto ‘Lakini nawaambia wale, wasiooa bado na wajane, Ni heri wakae kama mimi nilivyo, lakini ikiwa hawawezi kujizuia, na waoe, maana ni afadhali kuoa kuliko kuwaka tamaa’. Paulo aliona shida, maudhi ya wandugu walioko kwenye ndoa tokana na migogoro aliyokuwa akikutana nayo.
Fahamu kwamba ni furaha kubwa kwenye ufalme wa giza mtu anapooa au kuolewa kinyume cha mapenzi ya Mungu. Hii ni kwa sababu Shetani anajua akifanikiwa kukushawishi ukaoa kinyume na mapenzi ya Mungu, ameharibu ‘future’ yako na kile ambacho Mungu alikusudia ukifanye hapa duniani. Kumbuka suala sio kuoa au kuolewa tu, bali ni kuingia kwenye ndoa ambayo itakuwezesha kulitumika shauri la Bwana katika kizazi chako. Hivyo kabla hujaamua nani uishi naye hakikisha unamshirikisha Mungu akuongoze kumpata mwenzi sahihi.
  • Unapaswa kuoa au kulewa katika mapenzi ya Mungu
Naam kuoa au kuolewa katika mapenzi ya Mungu ni changamoto nyingine kubwa kwa vijana wa kizazi cha leo. Naam hili ni eneo ambalo Mungu yupo makini sana kufuatilia nani atakuwa mwenzi wako wa maisha. Na upande wa pili nao, Shetani anapigana kwa juhudi kubwa ili kuvuruga kusudi la Mungu kupitia mtu au watu.
Ni vizuri ukafahamu kwamba unapotaka kufanya maamuzi ya kutaka kuoa au kuolewa, Shetani naye ataleta mawazo (mapenzi) yake ndani yako juu ya nani anafaa zaidi  kuwa mwenzi wako maisha. Lengo lake ni kuhakikisha anakuunganisha na mtu ambaye anajua kwa huyo atakumaliza kiroho na kihuduma kabisa. Suala sio kuwazuia msiende kanisani, bali ni kuhakikisha kile ambacho ungefanya kwa kuwa na mtu sahihi hakifanikiwi. Ukitaka kujua ukweli wa jambo hili, muulize Mchungaji wako, kesi nyingi anazokutana nazo kanisani kwake zinahusu nini, naamini atakujibu kimapana. Ni jukumu lako kuwa makini kufuatilia unatii wazo la nani, Mungu au Shetani?  
  • Vigezo vya kimwili ni silaha kubwa ya uharibifu
Vigezo vya kimwili ni moja ya silaha kubwa ambazo Shetani anazitumia kuwavuruga watu wengi waweze kuoa au kuolewa nje ya mapenzi ya Mungu kwao. Jifunze kufukiri na kutafsiri mambo au makusudi kama Mungu anavyotazama na kutafsiri. Na uwezo wa kufanya hili utaupata kwenye neno lake tu. Kwako mwanaume Mungu anapokupa mke anakupa Mlinzi na msaidizi. Na kwa mwanamke Mungu anakuwa amekupa kichwa. Ni muhimu sana kuchunga ni msaidizi, mlinzi au kichwa gani unataka kiunganishwe na maisha yako kwa njia ya ndoa.
  • Ndoa ni wajibu mkubwa
Ndani ya ndoa kuna wajibu mkubwa sana unaokusubiri kama baba au mama. Ndani ya ndoa muda na uhuru wako unabanwa na mwenzi wako. Ndoa inabana pia muda wa kuwa na Mungu wako. Na kwa wengi kwa kutaka kuwapendeza zaidi waume au wake zao, wamefarakana na Mungu, kwa sababu wamewapa waume au wake zao hata nafasi na muda wa Mungu kwenye maisha yao.
Usiingie ndani ya ndoa kwa fikra za uapnde mmoja. Naam ndoa ni wito wa mapungufu na uvumilivu ambao ni lazima uwe tayari kuchukuliana na mwenzi wako katika mapungufu yake. Kuna vitu hamtaweza kufanana na kwa sababu ya mapungufu yaliyopo kwa kila mmoja  unapaswa kutafakari kuhusu majukumu yanayokuja kwako kama mwanandoa, hekima na busara katika kuzikabili changamoto za ndoa, kama vile kuzaa au kutokuzaa, kutokujiweza katika masuala ya unyumba, matumizi ya fedha, tabia za mwenzi wako nk.
Haya ni mambo ya kuhakikisha unayaombea mapema ili kujenga msingi imara utakapoingia kwenye ndoa yako. Lakini nikutie moyo kwamba endapo utaoa au kuolewa katika mapenzi ya Mungu, yeye ni mwaminifu, atakuunganisha na mtu ambaye katika changamoto mtakazokutana nazo hazitawakwamisha wala kuwafanya mjute. Bali endapo Shetani ndiye ataongoza maamuzi yako, ni majuto makubwa sana (asomaye na afahamu).
Mungu akubariki, naamini ujumbe huu umeongezea mambo ya kutafakari na kuzingatia kabla ya kufanya uamuzi wa kuoa au kuolewa.

No comments:

Post a Comment